Mtaa unatangaza misa ni pisi kali ‘gredi wani’ Bongo

Muktasari:

  • Mpaka hapo watoto wanaongoza kipindi cha kwanza. Ni wa kishua hata kama wako kando na ‘tailizi’ za washua wao. Bi Mdashi wao alijua kucheza na kalenda zake. Akachanga karata zake vizuri. Mkeka ukatiki sasa anamsikilizia mdosi ateme fuba.

Ni agizo rasmi la mtaa la wenye mtaa. Pisi kutoka kitaa, ubongo wake ukiwa umehifadhi elimu ya kidato cha nne tu. Tumbo likihifadhi na kufyatua watoto wawili tu mpaka sasa. Hajazaa ili mradi kazaa. Kawabebea wana wenye nawe yao mjini.

Mpaka hapo watoto wanaongoza kipindi cha kwanza. Ni wa kishua hata kama wako kando na ‘tailizi’ za washua wao. Bi Mdashi wao alijua kucheza na kalenda zake. Akachanga karata zake vizuri. Mkeka ukatiki sasa anamsikilizia mdosi ateme fuba.

Unadhani wale masela wawili walizaa na poyoyo? No! Unamuonaje kwanza? Ni pisi ya kwenda kweli. Unavyojiweka ndivyo watu wanavyokuchukulia. Anajua ‘kujipozisheni’. Anakaa kwenye njia ambazo mpira lazima upite kisha yeye atupie. Beki ikimgusa tu penalti.

Watu wenye akili timamu hujitoa mhanga kwenye pisi yenye akili timamu. Huwezi kuweka mbolea kwenye shamba lenye viwavi jeshi. Huwezi kupanda bustani kwenye kokoto. Masela nao walijilipua kwake kwa sababu, ana sababu ya kumfanya mtu awe na sababu ya kujilipua kwake.

Pisi siyo ya kishua wala siyo ya kimjini mjini sana. Haipo anga za kina dada wa mjini kweli kweli. Kuna upepo ilipita nao ikiwa bado binti ukamsomba jumla jumla. Lakini utulivu, akili na kipawa cha uvumilivu wenye subira kinamuweka katika ‘klasi’ ya juu. Anapiga pesa.

Achana na hayo mengine. Nenda katika ukurasa wake, angalia ‘dilizi’ zilivyojaa. Kuna eneo amejiweka, eneo ambalo mademu wengi wa mjini wameshindwa. Kawaacha mbali sana kwa sasa, yeye yupo kileleni pale Kibo wengine wapo huku Same wanaulizia basi za kwenda Rombo.

Miaka kadhaa imepita sasa. Toka aibu kwa pisi kali hii ya Daslama mjini ijitokeze. Ni katika jiji lenye joto zaidi Tanzania. Namuongelea Hamisa Mobetto ‘Misa’. Baada ya Mondi kumkana ‘laivu’ redioni. Lilikuwa pigo kwa Misa, Mama Misa na Team Misa.

Mondi akaendelea kuinanga ‘Pisi’ hii. Akaitupia kila aina ya maneno. Akiapa kutembea kwa magoti mpaka ‘Sauzi’.  Kwenda kumuomba msamaha ‘Zari The Boss Lady’. Hii kauli ilikuwa kisu kikali kwenye mfupa wa Misa na waliokuwa nyuma yake. Unyama ulikuwa mwingi sana.

Hizi zilikuwa ni ‘badi momenti’ kwa Misa. Sidhani kama atasahau katika ‘laifu’ lake. Mtoto alipiga moyo konde. Kisha kwa moyo wa kijasiri akageuza ukurasa wa kitabu chake. Akaimarisha himaya ya biashara zake. Ukubwa wa jina ikawa freshi kinoma na siyo kinyonge tena.

‘Dilizi’ mezani kwake kila siku hazikuisha. ‘Tripu’ zikawa nyingi kuliko Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki. Leo Dubai kesho US. Halikuwa tena jambo la ajabu. Hata nyimbo alizotoa na kina Christian Bella, ilikuwa sehemu ya starehe zake siyo msako wa pesa.

Mara paap Misa huyu hapa tunamuona ana-roll na rapa staa kutoka ardhi ya Jay Z na Beyonce. Kule kwa Joe Biden. Msela mwenye ndevu nyingi, voko flani na flow za hatari. Namuongelea Rick Ross ‘The Boss’. Whaaaaat? Swali la mshangao likabaki kwa wanga mjini.

Kwamba Misa kajiweka kwa Rick Ross? Rick Ross huyu wa Marekani? Au Rick Ross wa kwenye video ya Twenti Parcent? Wanoko hawakutaka iwe kweli, walitamani iwe ndoto hivi. Mwanzo hakuna aliyeamini. Mwisho wameshusha kila kitu chini.

Kurasa kubwa za ‘Mtoni’ zikaripoti ukaribu wa ‘Misa na Rozee’. Bila kusubiri ushuhuda, nina uhakika Mond alibaki mdomo wazi. Na kabla hajafunga mdomo wake. Mtaa nao ukamtangaza rasmi Misa kwamba ndiye ‘Mrembo grade one Bongo kwa sasa’.

Hili ni agizo la mtaa na halipingwi. Ogopa sana kiumbe ambaye kafunga ndoa na mtaa. Hii hutokea kwa wachache sana. Kwa mbelembele walikuwepo kina Pablo Escobar na wahuni wengine katika vitongoji vya Chile, Colombia, Queens New York nk.

Mtaa umefunga ndoa na Misa, ndiyo maana kila anachogusa kinageuka dhahabu. Raia wanamkubali ndiyo maana ukurasa wake Insta una wafuasi wengi kuliko Gwajima. Hutaki weka naye ‘bato’ uone ‘back up’ anayopewa na kitaa.

Ukiuteka mtaa umemaliza kila kitu. Mitaa ndiyo inayotupa maisha.