Rihanna aikacha 'Met Gala' 2024

Muktasari:

  • Kwa mujibu wa tovuti ya People imeeleza kuwa ilimtafuta mmoja wa watu wa karibu wa Riri ambapo alidai kuwa mwanamuziki huyo aliamua kughairisha kuhudhuria tamasha hilo kutokana na kuumwa na mafua.

Wakati wadau mbalimbali wakisubiri kuona muonekano wa mwanamuziki Rihanna katika usiku wa tamasha la mitindo duniani ‘Met Gala’  lililofanyika katika ukumbi wa  ‘Metropolitan Museum of Art’ Manhattan, New York City, nchini Marekani msanii huyo hakuweza kufika katika tamasha hilo kutokana na maradhi.

Kwa mujibu wa tovuti ya People imeeleza kuwa ilimtafuta mmoja wa watu wa karibu wa Riri ambapo alidai kuwa mwanamuziki huyo aliamua kughairisha kuhudhuria tamasha hilo kutokana na kuumwa na mafua.

Ikumbukwe kuwa siku chache zilizopita Rihanna wakati akiwa kwenye mahojiano na moja ya media alidai kuwa ‘Met Gala’ 2024 atavaa kawaida sana tofauti na miaka iliyopita huku akitoa sababu kuwa ameshakuwa mama hivyo hawezi kufanya vitendo alivyokuwa akivifanya katika tamasha hilo miaka ya nyuma.

Katika miaka ya nyuma, Rihanna (36), na mumewe A$AP Rocky (35), wamekuwa wakiwavutia wengi kupitia mavazi yao wanayovaa katika Met Gala huku wakijizolea sifa kutoka kwa mashabiki zao kutokana na ubunifu wa mavazi hayo.

Aidha mastaa wengine ambao hawakuonekana katika tamasha hilo na kufanya mashabiki kukata tamaa ni pamoja na Taylor Swift, Lady Gaga, Jared Leto, Blake Lively,Ryan Reynolds, Beyoncé, Billie Eilish na wengineo.