Suge: Diddy yupo hatarini

Muktasari:

  • Suge ameyasema hayo kupitia podcast yake ya ‘Collect Call’ ambayo anaifanya moja kwa moja akiwa gerezani ambapo amemshauri Diddy kujisalimisha kwani shutuma hizo tayari zimemletea tafsiri mbaya kwa jamii na kwa muziki wa Hip-Hop.

Mkurugenzi wa zamani wa ‘lebo’ ya Death Row Records, Suge Knight, amefunguka mengi kuhusiana na tuhuma zinazomkabili mkali wa Hip-Hop Diddy kwa kueleza kuwa Combos kwa sasa yupo hatarini, huku akidai kuwa mwanamuziki huyo anaweza kukutana na hali mbaya kama aliyokuwa nayo yeye gerezani.

Suge ameyasema hayo kupitia podcast yake ya ‘Collect Call’ ambayo anaifanya moja kwa moja akiwa gerezani ambapo amemshauri Diddy kujisalimisha kwani shutuma hizo tayari zimemletea tafsiri mbaya kwa jamii na kwa muziki wa Hip-Hop.

Suge anatumikia kifungo cha miaka 28 katika Gereza la Jimbo la California baada ya kukutwa na hatia ya kumgonga na kumuua Terry Carter na kumjeruhi Cle ‘Bone’ Sloan mwaka wa 2015.

Mwanzoni wa wiki hii mjengo wa Diddy uliopo Los Angeles ulifanyiwa upekuzi na Mawakala ya Usalama wa Taifa nchini Marekani ikiwa kama sehemu ya uchunguzi wa serikali kuhusu madai ya biashara ya ngono yanayomhusisha msanii huyo.

Aidha mpaka kufikia sasa bado haijabainishwa ni wapi msanii huyo yupo huku watoto wake wawili wakiume waliokuwa wakishikiliwa na polisi #Justin na King Combs, wakiondoka kwenye nyumba waliyokuwa wakiishi baada ya kuachiwa huru.