Watoto wa Mr. Ibu waiba pesa za matibabu ya baba yao

Muktasari:

  • Pesa zinazodaiwa kuibiwa ni zile ambazo Mr Ibu alikuwa amechangiwa na mashabiki kwa ajili ya kupatiwa matibabu ya ugonjwa uliokuwa ukimsumbua tangu mwaka jana.

Nigeria. Ama kweli kuzaa si kupata, ndivyo unavyoweza kuunga mkono usemi huo wa wahenga  kutokana na kitendo alichofanyiwa mwigizaji maarufu nchini Nigeria, John Okafor.

Onyeabuchi Okafor ambaye ni mtoto wa kiume wa muigizaji kutoka nchini Nigeria John Okafor, maarufu kama Mr Ibu na mtoto wa kike wa kuasili aitwaye Jasmine Okekeagwu, wamedakwa na Polisi nchini humo kwa madai ya kuiba fedha zilizokusanywa  kwa ajili ya matibabu ya muigizaji huyo.

Pesa zinazodaiwa kuibiwa ni zile ambazo Mr Ibu alikuwa amechangiwa na mashabiki kwa ajili ya kupatiwa matibabu ya ugonjwa uliokuwa ukimsumbua tangu mwaka jana.

Watoto hao wanadaiwa kuingia kwenye mifumo ya benki kwa kutumia simu ya muigizaji huyo waliyokuwa wakiimiliki na kuiba Naira 55 milioni ambazo ni zaidi ya shilingi 152.6 milioni.

Ikumbukwe kuwa Mr Ibu alikatwa mguu mmoja Novemba mwaka jana kutokana na ugonjwa unaomsumbua, ambao familia haijaweka wazi hadi leo.

Taarifa za kuugua muigizaji huyu zilianza kutolewa na mtoto wake huyo wa kike mwaka jana baada ya vyombo vya habari vya udaku nchini humo, kudai kuwa Mr Ibu amefariki hospitalini akiwa anapatiwa matibabu.

Katika kukanusha uvumi huo wa kifo, ndipo mtoto huyo aliomba msaada wa matibabu kwa mashabiki na kueleleza kuwa ukatwaji wa mguu kwa baba yake utakuwa ni kati ya upasuaji wa saba aliowahi kufanyiwa ili aendelea kuwa hai.

Mr Ibu amewahi kuigiza  movie kama 'The Collaborator' akiwa na Aki na Ukwa, 'Mr Ibu',  na 'My Chop Money'.