Dani Alves kuachiwa kwa dhamana ya Sh2.7 bilioni

Baada ya kutupwa jela miaka minne na nusu kwa makosa ya ubakaji, hatimaye Mahakama jijini Barcelona imesema itamwachia nyota wa soka wa zamani wa Brazil, Dani Alves kwa dhamana.

Taarifa iliyochapishwa na Washington Post imesema Alves ataachiwa iwapo atalipa dhamana ya Euro milioni moja sawa na Sh2.7 bilioni za Tanzania, sambamba na kukabidhi hati zake za kusafiria wakati akisubiri rufaa ya hukumu ya kumbaka mwanamke huko Barcelona.

Alves ambaye aliwahi kuchezea klabu za soka za Barcelona na PSG alipatikana na hatia Februari mwaka huu ambapo alihukumiwa miaka minne na nusu jela kwa kumbaka mwanamke katika klabu ya usiku mwaka 2022.

Nyota huyo mwenye umri wa miaka 40 amekuwa gerezani tangu akamatwe Januari 2023 huku maombi yake ya awali ya kuachiliwa kwa dhamana yakikataliwa kwa sababu mahakama ilimwona anataka kukimbia.

Wakili wake wa utetezi na mwendesha mashtaka wa Serikali wamekata rufaa dhidi ya hukumu hiyo.

Wakati wakili wake akitaka achiwe huru,  mwendesha mashtaka anataka kifungo chake kiongezwe hadi miaka tisa.