Aina za futari unazoweza kuandaa kwa dakika 30

Dar es Salaam. Katika kipindi hiki cha Mwezi Mtukufu wa Ramadhani kuna changamoto ya muda kwa wafanyakazi hususani wanawake.

Changamoto ya muda inatokana na kuwapo kwa muda maalumu wa kufuturu (kula) na chakula maalumu (futari).

Kutokana na changamoto hiyo leo ninakuletea futari mbili ambazo unaweza kuziandaa kwa muda mfupi.

Futari hizo ni pamoja na ndizi mbivu na viazi mbatata.

Futari ya ndizi mbivu

Mahitaji

Ndizi mbivu sita

Nazi pakiti moja

Sukari kiasi

Hiliki ya kutosha

  

Jinsi ya kutayarisha

Menya ndizi kisha toa moyo wa kati kati, zikate kate kulingana na unavyotaka, zipange ndani ya sufuria.

Weka maji kiasi kulingana na wingi na ugumu wa ndizi, zichemke kidogo  zikikaribia kuiva na kabla maji hayajakauka kabisa weka tui la nazi, mimina hiliki na sukari ziache zichemke hadi tui libaki kidogo, zitakuwa tayari kwa kuliwa.

Futari ya viazi mbatata

Mahitaji

Viazi mbatata kulingana na ukubwa wa familia ua watakaokula.

Nyanya

Vitunguu

Pili pili hoho

Karoti

Mafuta ya kupikia

Maji safi

Chumvi

Pili pili mtama 

 

Maandalizi

 

Menya viazi, unaweza kuvikata au kuviacha vizima kulingana na unavyopenda.

Vioshe vizuri kwa maji safi.

Tayarisha nyanya, vitunguu, hoho na karoti

Bandika sufuria ya kupikia jikoni, weka mafuta ya uto, yakichemka weka vitunguu maji, vikiiva kiasi weka vitunguu saumu, kisha acha viive hadi viwe na rangi ya hudhurungi (brown).

Weka viazi  mbatata kwenye mchanganyiko wa vitunguu koroga kwa muda na uviache kwa muda wa dakika 10 hadi 15 hadi vikaukie mafuta kisha weka nyanya hakikisha ukiweka nyanya moto uwe wa kutosha ili ziive.

Funika kwa dakika tano, geuza  kisha weka hoho na karoti kwa pamoja kisha funika, hapa unaweza kupunguza moto baada ya dakika mbili au tatu geuza na hakikisha vimechanganyika na vimebaki na mchuzi mzito kisha viipue tayari kwa kuliwa.