Mauaji ya wanandoa yazidi kushika kasi

Mwanza. Siku mbili baada ya kuripotiwa kutokea kwa kujinyonga kwa mkazi wa Kijiji cha Kizingwangoma wilayani Sengerema, Bernadeta Kulwa (28) kutokana na madai ya wivu wa mapenzi, mwanamke mwingine anatuhumiwa kumuua mumewe, Hosea Makoye (45) kwa kumchoma kisu tumboni.

Hili ni tukio la saba kwa wanandoa kuuana kwa takriban miezi mitatu kuanzia Aprili hadi sasa.

Kamanda wa Polisi Mkoa wa Mwanza, Ahmed Msangi alisema juzi saa tatu usiku katika Mtaa wa Magaka, Kata ya Kahama wilayani Ilemela, Makoye anadaiwa kuuawa na mkewe. Alisema Makoye alikuwa mfanyakazi wa Shirika la Umeme Tanzania (Tanesco) Mkoa wa Mwanza na kwamba, walikuwa na ugomvi wa mara kwa mara kwenye ndoa yao, mwanamke akidaiwa kutaka kurithi mali.