Mpina ‘akinukisha’ bungeni, aombwa ushahidi

Mbunge wa Kisesa (CCM), Luhaga Mpina akichangia kwenye makadirio ya mapato na matumizi ya Wizara ya Mifugo na Uvuvi kwa mwaka 2023/2024 leo Mei 3, 2023 bungeni jijini Dodoma. Picha na Merciful Munuo

Muktasari:

  • Mbunge wa Kisesa Luhaga Mpina (CCM) ameingia katika mgogoro na Bunge baada ya kutakiwa apeleke ushahidi wa namna gani Serikali imeshindwa kutekeleza maagizo ya Waziri Mkuu.

Dodoma. Mbunge wa Kisesa, Luhaga Mpina (CCM) ameingia katika mgogoro na Bunge baada ya kutakiwa apeleke ushahidi wa namna gani Serikali imeshindwa kutekeleza maagizo ya Waziri Mkuu.

 Mpina ambaye amekuwa mwiba kwa viongozi wa Serikali hasa mawaziri, jana Jumatano Mei 3, 2023 amemgusa Waziri Mkuu kwamba maelekezo anayoyatoa hayafanyiwi kazi lakini akahoji ni kwa nini amekuwa kimya.

Akichangia katika Hotuba ya Waziri wa Mifugo na Uvuvi kwenye maombi ya fedha kwa mwaka 2023/24, Mpina ambaye aliwahi kuwa Waziri wa Mifugo na Uvuvi (2017 -2020) ameelezea masikitiko yake kuhusu alichokiita ni kamatakamata ya mifugo bila utaratibu.

Hata hivyo wakati akichangia, Waziri wa Katiba na Sheria, Dk Damas Ndumbaro ameomba kumpa taarifa akieleza kuwa mbunge huyo ametumia vibaya jina la Waziri Mkuu kwa madai maagizo yake yanatekelezwa.

Mwingine aliyeomba utaratibu alikuwa Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu, Jenista Mhagama ambaye amesema kuwa mchango wa mbunge huyo umetuhumu mtu ambaye maagizo na maelekezo yake yameanza kufanyiwa kazi na watumishi ikiwemo mawaziri ndani ya Serikali.

Mpina alipopewa nafasi amesisitiza kuwa anao ushahidi wa kwa nini anasema kuwa maagizo hayafanyiwi kazi na akasema anaweza kuwasilisha ushahidi wa namna hiyo kwa Spika.

Kwa upande wake, Spika Dk Tulia Ackson amemuomba mbunge huyo kumpelekea ushahidi huo, ndipo atatoa mwongozo wake dhidi ya kauli ya Mpina.