Pauline Gekul afunguliwa kesi

Muktasari:

  • Wakili wa Kujitegemea Peter Madeleka amesema kesi hiyo ameifungulia mtandaoni.

Dar es Salaam. Wakili wa kujitegemea Peter Madeleka amefungua kesi ya jinai ambayo bado haijapewa namba, akimshitaki mbunge wa Babati Mjini, Pauline Gekul kwa madai ya kumshambulia na kumdhuru Hashim Ally Novemba 11, 2023 kinyume cha kifungu cha 241 cha Kanuni ya Adhabu Sura ya 16 ya 2022.

 Hata hivyo, Gekul aliyekuwa Naibu Waziri wa Katiba na Sheria kabla ya kutenguliwa Novemba 25, 2023, alipoulizwa kwa simu leo, amesema hana taarifa za kufunguliwa kesi.

Akizungumza na Mwananchi jana Jumamosi Desemba 9, 2023 Madeleka amesema kesi hiyo ameifungulia mtandaoni na hatua inayofuata ni kwenda kuipa namba.

“Sheria ya Mwenendo wa Makosa ya Jinai (CPA) kifungu cha 128(2) na (4) kinatoa ruhusa ya mtu kufungua makosa ya jinai,” amesema.

“Hatua ya kwanza ya kufungua kesi imekamilika. Natarajia Mahakama ya Wilaya ya Babati itatimiza wajibu wake kwa wakati ili kuanzia Jumatatu Desemba 11, 2023 hatua nyingine za kisheria ziendelee,” amesema Madeleka.

Katika hati ya mashitaka, ambayo Mwananchi imeiona, inadaiwa kuwa Gekul na watu wengine ambao hawamo kwenye hati hiyo, wakiwa wilayani Babati  walimwita Ally na kumshinikiza kwa bunduki, kumweka ndani, walimvua nguo na kumlazimisha kukalia chupa tupu ili ipenye kwenye tundu la haja kubwa wakijua kwamba matendo hayo ni kinyume cha sheria za Tanzania.