|
LAKINI ATAKA AWATIMUE MAWAZIRI, WASAIDIZI WANAOMUANGUSHA Julieth Kulangwa MIAKA minne iliyopita Askofu Methedious Kilaini wa Kanisa Katoliki alimuelezea Rais Jakaya Kikwete kuwa ni "chaguo la Mungu" na hadi sasa hajabadili msimamo wake, lakini anasema wasaidizi wake na mawaziri wake wanamuangusha na hana budi kuachana nao iwapo atachaguliwa tena kuongoza nchi. “Mwaka 2005 niliwahi kusema kuwa Kikwete ni chaguo la Mungu... kwa maana kwamba kiongozi yeyote anayechaguliwa na watu anakuwa amesimamishwa na Mungu," alisema Kilaini katika mazungumzo na Mwananchi Jumapili. "Miaka minne baadaye ameendelea kupendwa kwa kiasi kilekile na wananchi kwa kuwa kweli ni chaguo hasa ambalo Watanzania walilihitaji.”
Askofu Kilaini ametoa kauli hiyo wakati Rais Kikwete akiangaliwa kwa mtazamo tofauti katika kipindi ambacho anaelekea kumaliza kipindi cha miaka mitano cha utawala wake, na hasa baada ya kutoa kauli kali dhidi ya wafanyakazi mapema mwezi huu.
Serikali ya JK pia iliingia kwenye mgogoro mkubwa na viongozi wa kidini katikati ya mwaka jana baada ya bajeti kuu kuonyesha kuwa taasisi hizo zimefutiwa msamaha wa kodi uliokuwa unatolewa kwenye vifaa mbalimbali vinavyoingizwa kwa ajili yab huduma, kiasi cha Waziri Mkuu Mizengo Pinda kulazimika kufanya mikutano ya haraka iliyomalizika kwa msamaha huo kurejeshwa.
Lakini Askofu Kilaini anaona kuwa mapungufu yaliyoibuka kwenye serikali ya JK yalitokana na udhaifu wa mawaziri na wasaidizi wake.
“Yapo mambo ambayo hayakwenda vizuri katika kipindi hiki, lakini ukiangalia yeye kama rais hawezi kujua kila kitu... anahitaji kusaidiwa na watendaji wake wa karibu na hawa wamekuwa wakimwangusha mara kwa mara," alisema Askofu Kilaini katika mahojiano na Mwananchi Jumapili. Kiongozi huyo wa kiroho alisema wapo baadhi ya mawaziri ambao hawajamsaidia rais wala kutimiza wajibu wao kwa nyadhifa walizopewa na kwamba hao ndio waliochangia kuitia doa serikali ya Kikwete. “Wapo mawaziri ambao hawajafanya chochote tangu alipowateua," alisema askofu huyo ingawa hakuwa tayari kuwataja mawaziri hao.
"Inafikia wakati rais au waziri mkuu analazimika kufanya majukumu yao (ya mawaziri hao). Hawa hawamfai na rais inabidi asiwateue tena baada ya uchaguzi ujao.”
Askofu huyo, ambaye amekuwa hasiti kuzungumzia masuala mbalimbali kila anapotakiwa kufanya hivyo na vyombo vya habari, pia aligeukia wasaidizi wake na kueleza kuwa kwa kiasi kikubwa ndio waliochangia kumwangusha JK. Alisema rais hawezi kujua kama hoteli anayokwenda kuizindua imejengwa kwenye hifadhi ya barabarani, alisema Kilaini akirejea tukio la hoteli ya kitalii ya Arusha ambayo Kikwete aliifungua rasmi na sikku moja baadaye ofisi ya Wakala wa Barabara (Tanroads) mkoani Arusha ikavunja ukuta wa uzio kwa sababu ulijengwa ndani ya hifadhi ya barabara. "Ni kazi ambayo ilitakiwa kufanywa na watu ambao wanalipwa mishahara mikubwa inayotokana na fedha za walipa kodi. Hawa wamekuwa wakimwangusha kwa kumuingiza katika mambo yasiyofaa," alisema Kilaini. Awali akifafanua sababu za kuendelea na msimamo wake kuwa Rais Kikwete ni kipenzi cha wengi, Askofu Kilaini alisema kuwa kiongozi huyo wa serikali ya awamu ya nne amekuwa karibu na wananchi, hivyo si vibaya wakampa tena nafasi ya kuongoza nchi.
Lakini, Kilaini ambaye ni askofu msaidizi wa jimbo la Bukoba, aliliambia gazeti hili kuwa katika kipindi cha utawala wake wa miaka minne iliyopita, Rais Kikwete alijiweka karibu na wananchi ndio maana ameendelea kupendwa. Askofu huyo, mwenye msimamo wa wastani dhidi ya serikali, aliongeza kwamba Kikwete anapendwa kwa kuwa ni rais aliyejiweka karibu na jamii tofauti na marais wengine, hali iliyosababisha kupendwa na wananchi. Kilaini alimsifu Kikwete kuwa ni rais pekee aliyefungua milango ya ukweli na uwazi kwa kuacha kila kitu kizungumzwe na kuchambuliwa kwenye vyombo vya habari kwa mapana yake bila mipaka.
“Ni Rais aliyeruhusu uhuru wa kuongea; vyombo vya habari vinaandika na watu wanazungumza kila kitu bila kuingiliwa au kunyamazishwa. Kwa dhamana aliyonayo angeweza kuzuia mambo haya, lakini anaawaacha watu wachambue mambo yanayowahusu mpaka ukweli utakapopatikana," alisema. Aliongeza kusema: "Mfano, kuna habari iliwahi kuandikwa na gazeti moja kuwa Rais Kikwete alinilipia matibabu nchini India wakati fulani nilipougua. Haikuwa habari ya kweli, lakini rais hakutaka kulizungumzia na kuwaachia walioanzisha walimalize.”
Alisema kwa uhuru huo alioutoa mkuu huyo wa nchi, umemfanya kuwa mmoja kati ya marais walioandikwa sana na vyombo vya habari na kushambuliwa na vyama vya siasa.
Kilaini aliongeza kwamba Rais Kikwete anapaswa kuendelea kuongoza hasa kutokana na uwezo mkubwa aliouonyesha katika suala la kuushugulikia mgogoro wa kisiasa wa Zanzibar. “Suala la Zanzibar lilikuwa gumu na hakuna aliyefikiri kama angeweza kulishughulikia na kulifikisha hapa lilipo katika kipindi kimoja tu... kwa hili amejitahidi na kwa kweli anahitaji msaada ili nchi yetu iendelee kuwa kisiwa cha amani ulimwenguni,” aliasa Watanzania.
|
Comments
Baba askofu ni binaadamu na mchungaji pia. Kuna wakati anatoa maoni kama mtu mwingine na kuna wakati anazungumza katika kiti chake cha uchungaji. Kama binaadamu pia askofu ana haki na uhuru wa kumpigia kura mtu na chama chochote anachokipenda lakini hana haki ya kuwachagulia waumuni wake kiongozi iwe moja kwa moja au kwa taathira. Hata hivyo, kiongozi anaposhinda uchaguzi na kuwa kwa mfano, raisi, askofu pamoja na taasisi yake wakiwa kama subjects ya dola wanawajibika kuikubali na kuitii dola iliyopo madarakani. Ndipo hapo dhana ya viongozi ni chaguo la Mungu inapokuja. Nadhani baba askofu alikuwa anamaanisha dhana hii ya pili.
Kwa ujumla nakubaliana na wachangiaji wote kwamba viongozi wa dini hawapaswi kuwachagulia waumini wao chama au kiongozi. Naamini pia, viongozi wa dini ni mahiri na wameandaliwa zaidi katika anga zao za kidini. Katika fani nyingine kama siasa ni watu kama sisi na wengine hawana elimu na taarifa ya kutosha katika siasa. Waumini tunapaswa kuwaheshimu na kuwafuata katika mambo ya kidini. Wakiingia katika anga za siasa tupambane nao kama watu wa kawaida tu na hamna dhambi yoyote tutakayopata.
Mnapotosha waumini, kwa faida au maslahi binafsi hiyo ni dhambi kubwa. ACHA KABISA KUSEMA NI CHAGUO LA MUNGU.
Nchi haieleweki inaelekea wapi, leo dola ni sh 1400- 1500, sababu kubwa ni pesa za ujanja ujanja za kifisadi kuwepo mtaani chini ya usimamizi wa JK, bora ningekuelewa ungesema Baba wa Taif ni chaguo lakini sio huyu. Tafadhali tafuta cha kufanya kama umekosa acha kabisa siasa.
JK kaja marekani mara ngapi? serikali imelipa kiasi gani? je tumepata faida kwa yeye kuja huku? Walimu, wauguzi wanaumia wewe unasema ni chaguo la Mungu, angalia watu huacha kwenda kusali sababu nyingine ni kama hizi. ACHA KABISA NAKUHESHIMU BABA ASKOFU, ACHA KUMUHUSISHA MUNGU NA WATU WA NAMNA HII. Kuchaguliwa na wengi kwa u[NENO BAYA] sio Mungu, chaguzi zenyewe mizengwe tupu. MIMI UMENIKWAZA SIPENDI.
Wengi nadhani wanashindwa kumwelewa Baba Askofu Kilani. Anabadilika badilika kama kinyonga!!!