
| Ushindi wa Shein wazua vurugu Z'bar | Send to a friend |
| Sunday, 11 July 2010 10:12 |
|
Na Waandishi Wetu UTEUZI wa Dk Ali Mohammed Shein kuwa mgombea urais wa Zanzibar kupitia CCM umepokelewa kwa vurugu visiwani (Zanzibar) na baadhi ya wanachama wa chama hicho wakipinga uteuzi huo.Wakati huko Zanzibar hali ikiwa tete, baadhi ya wakazi wa Tanzania Bara wameuunga mkono uteuzi huo wakisema utamaliza siasa za chuki visiwani. Mara baada ya kupata taarifa za uteuzi huo kutoka mjini Dodoma, wanachama hao waliokuwa katika maeneo mbalimbali ya Unguja walipandwa hasira na wengine kutamka wazi kuwa hawatamuunga mkono Dk Shein katika kampeni za uchaguzi mkuu . Baadhi yao wakiwa katika maeneo ya starehe, kama vilabu vya pombe, walivunja chupa ukutani kuonyesha hasira zao kupinga kutoteuliwa Dk Mohammed Gharib Bilal au Shamsi Vuai Nahodha katika nafasi hiyo. Maeneo ambayo watu hao walikuwapo huku wakifuatilia mkutano wa Dodoma ni pamoja na mitaa ya Maisara, Gofu, Kwa-Raju, Ghymkana na Hoteli ya Bwawani ambayo mwishoni mwa wiki hujaa wageni wanaoenda kwa ajili ya starehe. “Hatujafurahi hata kidogo, lakini hatuna la kufanya na hii kuvunja chupa ni kuonyesha hasira zetu kwa sababu chaguo la Wazanzibari tokea uchukuaji wa fomu za urais wa CCM ni Dk Bilal,” alisema Kijana mmoja. Juzi Halmashauari kuu ya CCM, ilimtangaza Dk Shein kuwa mshindi baada ya kupata kura 117 na kuwashinda wapinzani wake Nahodha aliyepata kura 33 na Dk Bilal ambaye alipewa nafasi kubwa ya kupitishwa akaambulia kura 55. Mjini Dodoma mara baada ya kutangzwa matokeoa hayo, wafuasia Dk Bilal na Vuai walikchukia, baadhi yao walitupa kofia na mashati ya CCM nje ya ofisi za chama makao makuu na kuahidi kutoshiriki katika kampeni za kumnadi Shein. Wana CCM, hao zaidi ya 200 ambao waliondoka jana asubuhi mjini hapa na kurejea Zanzibar, walisema wamechoka kuchaguliwa Rais wa Zanzibar na viongozi wa CCM Tanzania bara na sasa wanataka mabadiliko katika Katiba ya CCM, ili Rais wa Zanzibar achaguliwe na Wazanzibar wenyewe. "Hatutaki..., huyo siyo mgombea wetu…, tumechoka kuchaguliwa Rais Zanzibar,” umati wa wanaCCM toka Zanzibar ulipiga kelele mara baada ya taarifa kuvuja kuwa Dk Bilal na Nahodha hawakuchaguliwa. “CCM Zanzibar imekufa na sasa bora CUF ichukuwe nchi," walisema wanaCCM hao. Akizungumza na Mwananchi Jumapili kada wa CCM Zanzibar, Baraka Mohamed Shamte aliyewahi kuwa katibu wa CCM wilaya za Wete, Unguja mjini na Pangani mkoani Tanga, alisema hawakuridhika na matokeo ya kura za wajumbe wa halmashauri kuu, sasa wameamua watafanya mgomo baridi wa kususia shughuli za CCM na kampeni. "Kwanza mgombea mwenyewe sisi hatumkubali, kwa vile hana kura Zanzibar,"alisema Shamte. Hata hivyo, dalili za kutopata kura za kutosha kwa Bilal na Nahodha, zilianza kuonekana mara baada ya kuanza kikao cha halmashauri kuu ambapo wajumbe wengi wa bara walionesha wazi kutaka kupiga kura za kiitifaki na kumpa ushindi Shein. Katika kuhesabu kura Dk Bilal alimteua Mbunge wa Same Mashariki, Anna Kilango kumhesabia jambo ambalo liliwashangaza wengi. Licha ya wafuasi wa Dk Bilal wengi wao wakiwa ni akina mama na vijana wa maskani mbalimbali, kwa takriban siku tatu walikuwa wakipiga kampeni nzito ya katika nyumba za kulala wageni hasa wajumbe wa NEC, hali ilibadilishwa ukumbini taarifa ya kuvuja taarifa za kamati kuu kuwa jina la Shein ndio liliongoza. Uchunguzi wa Mwananchi Jumapili katika mji wa Zanzibar ulibaini usiku mzima wa juzi na jana asubuhi vijiwe kadhaa vilikuwa kimya, kuashiria hali ya huzuni. Vijiwe vya kahawa na maskani za CCM ikiwemo ya Kaka ya Kisonge ambayo hutawaliwa na shamra shamra wakati wa uteuzi wa mgombea urais vilikuwa kimya. Mazingira ya ukimya katika maskani za CCM jana mjini hapa zilifuatiwa na kuwasili kimyakimya kundi la wana CCM waliosusa kikao ambalo lilikuwa likimuunga mkono Dk Bilal na Nahodha. Baadhi ya wana CCM hao waliozungumza na gazeti hili mara baada ya kuwasilia kutoka Dodoma , walisema hawakuridhishwa na mchakato mzima wa uchaguzi na wanaimani kwamba, kuna njama zilizofanywa na CCM bara katika kuteua mtu ambaye wao wanamtaka. Baraka Shamte ambaye ni mwana CCM alisema katiba ya CCM ni mizengwe na inahitaji mabadiliko ya haraka ili Wazanzibari wasichaguliwe kiongozi wao na watu kutoka Tanzania bara. “Tumepokea uteuzi wa Shein shingo upande na baadhi yetu hatushiriki katika harakati zozote za kampeni ya uchaguzi kwa sababu sio chaguo letu. Lazima katiba ya chama ibadilishwe wazanzibari tusichaguliwe kiongozi,” alisema kwa hasira Shamte. Alisema hata kama Dk Bilal atapewa nafasi nyingine ya juu kama vile makamu wa rais bado kiu yao haijamalizika kwa kuwa lengo lao ni kutaka awatumikie Wazanzibar na sio jamhuri ya muungano wa Tanzania. Naye Said Hassan alisema utaratibu wa kuchagua rais ndani ya chama Zanzibar lazima limalizikie Zanzibar kwa vile, jambo hilo linawahusu Wazanzibari wenyewe. Mmoja wa wafuasi hao ambaye hakupenda kutajwa jina lake, alisema wanajipanga kuangalia mustakabali wao katika CCM na kwamba, ikiwezekana wanaweza kuondoka. “Tuna masikitiko makubwa kwamba hatutaweza kuzungumza nanyi (waandishi) kwani tumepokea maagizo kuwa tusizungumze chochote kuhusiana na matokeo ya uchaguzi Dodoma. Hivi sasa tunakwenda zetu nyumbani tukiwa na huzuni kubwa,” alisema mfuasi mmoja ambaye hakutaka kutajwa jina lake gazetini. Taarifa za awali zilizosambazwa kwa vyombo vya habari Zanzibar zinasema kundi hilo la wafuasi wa Dk Bilal lililotoka Dodoma lilipanga kunfanya mkutano na waandishi wa habari baada ya kuwasilia saa 9:30 bandarini, lakini baadhi yao walieleza kuwa wamepokea taarifa kutoka Dodoma kwamba, wasizungumze lolote. Baadhi ya wafuasi hao walikataa kutii agizo hilo wakilalamika kuwa hawakutendewa haki na kutishia kukihama chama na kwamba, waandishi wa habari wahudhurie siku ya kurejesha kadi zao za CCM kwa chama watakachojiunga ambacho watakitaja baadaye. Mashabiki hao walionekana wakiwa na hasira kubwa walidai hata sare za CCM walizivua mjini Dodoma mara baada ya kutangazwa Dk Shein. “Tunaomba waandishi mtupe muda zaidi mtapata baadaye na tunaomba hizo kamera zenu kwanza wekeni chini kwa sababu hatutaki kupigwa picha. "Chama kimetuangusha na kimetuvunja moyo sana wana CCM Zanzibar na tunajitayarisha kurudisha kadi za CCM, lakini kwanza hatusemi tutajiunga chama gani,” walisema mashabiki hao huku wengine wakiwa wamejifunika nyuso zao. Hata hivyo, baadhi ya wananchi wazanzibar wakiwemo wana CCM wanaounga mkono maridhiano wamepokea kwa furaha uteuzi wa Dk Shein wakisema ni kiongozi pekee atakayeweza kuwaunganisha Wazanzibari. “Tumefurahi sana na tumepokea uamuzi wa Nec kwa furaha ingawa wengine wamekasirika kama mnavyoona. Lakini sisi tumefurahi na tunaomba wana CCM wenzetu tuungane ili tujenge chama chetu, tusiwape mwanya wapinzani wetu,” alisema Omar Ali Haji. Kutoka Mwanza, Fredick Katulanda anaripoti kuwa baadhi ya wakazi wa mji huo wamesema kuteuliwa kwa Dk Shein kutamaliza makundi ndani ya CCM, hivyo kuifanya Zanzibar kuwa tulivu katika uchaguzi mkuu wa mwaka huu. Makamu Mwenyekiti wa TCCIA Taifa, Amran Batenga alisema kuteuliwa kwa Shein kunaweza kumaliza makundi ambayo yamekuwa yakisumbua kila mara katika siasa za Zanzibar. “Mimi naona ni uteuzi mzuri, wameteua mtu ambaye haoneshi kuwa na makundi, wameteua mtu kutoka Pemba, safi, nadhani CCM imedhamiria katika uchaguzi huu kukomesha Upemba na Uunguja,” alieleza Batenga. Naye Mwita Frank alisema ameupokea uteuzi huo wa CCM kumteua Dk Shein kama ishara ya kushindwa na kuanguka kwa CUF kwa vile kila mwaka wa uchaguzi kimekuwa kikitumia nguvu ya wananchi wa Pemba kujinadi. Naye, Jumanne Isaya alisema uteuzi huo wa CCM umepotea njia kwa vile utatoa nafasi ngumu ya CCM kuishinda CUF kutoka na uteuzi kuzaa makundi kwa vile Wazanzibari wanaamini kuwa Dk Shein ni changuo la bara na siyo lao Zanzibar “Ni uteuzi mzuri kwa vile ni mtu makini, lakini kwa siasa za Zanzibar bado naona hawajatibu kitu, utazuka mvutano kwa sababu wao wanaamini kuwa uteuzi wake unashinikizo la CCM Bara na wala siyo la CCM Zanzibar” alieleza. Kutoka mkoani Mara, Imeripotiwa kuteuliwa kwa Dk Shein kuwania nafasi ya urais kupitia CCM, kumepokelewa kwa hisia na mitazamo tofauti. Akielezea uteuzi huo, Paroko wa Kanisa Katoliki Parokia ya Mugumu wilayani Serengeti Padri Aloyce Magabe alisema CCM wametumia hekima kumteua Dk Shein kwa kuwa ni miongoni mwa viongozi waliolitumikia Taifa hili bila kukumbwa na tuhuma za ufisadi. "Huyu ni chaguo la watu na hata Mungu maana hajawahi kukutwa na tuhuma, amekuwa akishughulikia mambo kwa utulivu," alisema. Padri Magabe ambaye ni mchambuzi wa mambo mbalimbali alisema ana imini kuwa Shein atuweza mzigo huo kwa kuwa tayari ana uzoefu kwa vipindi viwili akimsaidia Rais wa Jamhuri ya Muungano na kwa kuwa anatoka Pemba basi. Kutoka Bukoba imeripotiwa kwamba baadhi ya wazee wa mji wa Bukoba limeishauri kuwa kundi la mgombea aliyeshindwa kudhibitiwa ndani ya chama kwa vile linaweza kuendesha kampeni chafu ili kumharibia Dk Shein katika uchaguzi. Walisema kundi la Dk Bilali linaweza kuibuka kutokana na ukweli kuwa lilikuwa na nguvu na lilishajiwekea matumaini ya kushinda katika mchakato huo hivyo huenda likawa na kinyongo. Miongoni mwa wazee hao Justus Mutalemwa alisema matokeo yaliyompa ushindi Dk Shein yanaonyesha pia wapinzani wake walikuwa na nguvu hali aliyosema huenda ikaleta mazingira magumu ya kisiasa kisiwani humo. Mathias Balige, mkazi wa Hamuembe mjini Bukoba alisema kulikuwa na mazingira ya wazi ya baadhi ya viongozi ndani ya chama kumbeba mgombea aliyeshinda. Alisema hali hiyo huenda ikazidi kuchochea chuki na kufanya kampeini za kumnadi mgombea huyo kutiwa dosari katika uchaguzi. Balige alisema huenda ukatokea mgawanyiko mkubwa kuelekea katika kipindi cha kampeini. Alipoulizwa kama mgombea huyo ataweza kuwaunganisha Wazanzibari na kuyavunja makundi yenye uhasama, alisema sio rahisi kumaliza nguvu ya makundi yenye uhasama kwa kuwa mtandao wa kundi lake umehusika kumpatia ushindi. Wakati huo huo, Katibu Wakati huo huo; Mkuu wa CUF, Maalim Seif Sharif Hamad, amempongeza Dk Shein kwa kuteuliwa na Halmashauri Kuu ya CCM kuwa mgombea wa urais kupitia chama hicho. “Nampongeza Dk Shein kwa kuchaguliwa kwa kura nyingi…hii inaonyesha imani waliyonayo wanachama wenzake wa CCM kwake na uongozi wake…binafsi nimepokea uteuzi wake kwa furaha kubwa sana,” alisema Seif ambaye atashindana na Dk Shein katika uchaguzi mkuu. Katika taarifa yake, iliyotolewa na msaidizi wake, Ismail Jusa, Seif alisema anaamini Dk Shein ni mtu makini, msomi, mwenye uwezo, busara, hekima na asiyependa makuu. Alisema kutokana na sifa hizo, anaamini Dk Shein ataweza kuondoa makundi ndani ya chama chake. “Kupatikana kwa umoja ndani ya CCM kutamwezesha Dk Shein kushirikiana na sisi na vyama vingine vyote vya siasa ili, kwa pamoja, tujenge umoja mpana zaidi kwa Wazanzibari wote,” alisema. Kiongozi huyo wa CUF alisema ametiwa moyo sana kwa kauli ya Dk Shein kuwa anaunga mkono na atatekeleza na kuendeleza maridhiano yaliyoanzishwa na Amani Karume na yeye (Seif). Alisema anaamini kwa hulka yake, Dk Shein na yeye kwa pamoja, wataweza kuleta siasa mpya za maelewano kwa Wazanzibari wote, zenye lengo la kuleta maendeleo makubwa na ya haraka. Habari hii imeandaliwa na Salma Said - Zanzibar, Phinias Bashaya - Bukoba na Frederick Katulanda - Mwanza na Samuel Kamndaya Dar. |
| Last Updated on Sunday, 11 July 2010 10:14 |

Habari Mpya
Picha
Zenye Mvuto
- Nafasi za Kazi
- Links za wateja na washirika wetu
- Muswada wa madini waitoa jasho serikali
- Bi kizee asafari kilometa 50 kupinga hotuba ya JK, AMUONYA ASITUMIE MADARAKA YAKE VIBAYA
- Mishahara sekta binafsi Tucta yashtukia danganya toto
- Vigogo UVCCM wajiuzulu
- Mwinyi atetea ajira za wafanyakazi, ashauri utu uheshimiwe kudumisha Amani


UTEUZI wa Dk Ali Mohammed Shein kuwa mgombea urais wa Zanzibar kupitia CCM umepokelewa kwa vurugu visiwani (Zanzibar) na baadhi ya wanachama wa chama hicho wakipinga uteuzi huo.












Comments
UTEUZI WA MGOMBEA WA URAIS SAFARI HII NI MWIBA KWA WALE WASIOITAKIA MEMA ZANZIBAR WANZANZIBARI WAMEBAGULIWA NA KUNYANYASWA KWA SABABU YA ASILI ZAO TU .
DKT BILALI ALIKUA NI MTU MAKINI NA WA KUHESHIMIKA ALIUNGANA NA GENGE LA KISHAMBA KINA SALMINI WAKAIHARIBU ZANZIBAR KWA CHUKI NA UBAGUZI TUNA MSHUKURU MOLA KARUME ALIWAPIGA NA CHINI WOTE WAKABAKI WASIJUE LA KUFANYA BILALI ALIRUDI CHUONI KUFUNDISHA ,SALMINI HAJULIKANI MBELE WALA NYUMA JUZI KAINGIA DODOMA NA SARE ZA CUF BLUE GUARD HATA ZA CCM ZILIMSHINDA KUVAA.
DKT BILALI HAKUWA NA NIA YA KULETA UONGOZI MWEMA ZNZ ALIKUA NA LENGO KUJA KULIPIZA KISASI KWA UONGOZI WA KARUME LAKINI KASAHAU KARUME NI MTOTO WA MJINI . BILAI MSHUKURU MOLA WAKUPA FAVOUR KUBWA JIANAGALIE AFYA YAKO KWANZA UMECHOKA KINOMA INABILI CCM WAKUSAIDIE TENA WAKUFANYIE SERVICE YA NGUVU MEDICAL ! UMEWAACHIA WAKATI MGUMU WAHUNI WA KISONGE NA WENGINE FAGIO LA CHUMA LINAKUJA SOMA WAKATI. MUNGU IBARIKI ZNZ.
Sifa kubwa ya Shein ni mtu ambaye hana makundi yeye yupo na anfuata katiba na mwongozo wa chama chake kwamba sasa tunataka nini natufanye nini ili tuweze kusonga mbele.
Zanzaibar wamepata kiongozi mzuri na mwadilifu na mwenye kuwatumikia wananchi hasa wazanzibar maana alivyokuwa makamu wa rais tumeona akiongoza kwa busara bila kusikia kelele wala ugomvi na mtu yeyote ndani ya ccm na nje ya ccm.
yoyote yule kiongozi aloyechaguliwa inatakiwa awajibike na mambo hayo.
kuleta mabadiliko, unafuu wa maisha upatikane, sio mengine, lakini viongozi wengi wa tanzania wao ni kujilimbikizia mali tu, kuiba fedha za umaa tu, kuanzia ngazi ya wakurugenzi hadi raisi mwenyewe,
jee hiii kweli tutafika?
mimi nafikiri Tanzania haita endelea hadi mwisho wa dunia itakuwa ni hivi hivi tu, watu kupishana ,urais, kaa miaka kumi yako hiyo, kula iba, nyanganya, ukimaliza akae mwengine ,na kundi lake nao wanyinufaishe wao na familia zao, hadi mwisho wa dunia.
Ukweli ni kuwa karibu Viongozi wote khutembea nchi za wenzetu huona yale mazuri , ya maaana na maendeleo . huwa hawayachukui wakaja kuwasaidia wananchi wao nao wafaidike, yaani ziara za nje ni shopping na kutembea tu.
kwa kweli awe Shein, awe bilal, wananchi wanachotaka ni kuwaondolea ugumu wa maisha, na kubuni njia za kuleta b maendeleo ya nchi.
Hao wote ni Viongozi, kila mmoja ana taaluma tofauti na zote taaluma zao ni muhimu na zinafaa, haina haja ya kuwabagua,
kama lengo ni maendeleo basi ni kushirikiana kuleta hayo maendeleo ya kweli,
nadhani inatosha tujengeni nchi wenzangu,
tusichague sanaaa, tushirikiane tujenge nchi
tusikae tuaakamini labda siku moja tanzania itakuwa kama ulaya hiyo katu.
wenzetu wanajituma viongozi wanawajibika, wankwenda mbele sii wizi na kwenda mbele
tuaache tujenge nchi
hii ni ccm kutaka kuwazima wazanzibar tu na sio jengine. KUMBUKA KWAMBA DR AMETUMWA NA WAZANZIBAR NA SIO MTU MWENYE UCHU WA MADARAKA BALI ALIKUA ANAITIKIA WITO, hata hivyo ni bora tufunike kombe mwanaharamu apite tusijaribu ku[NENO BAYA]noa mambo kwani sio jambo jema. yalopita sio ndwele na tugange yajayo.kamati kuu ya chama sio wapiga kura wapiga kura ni hao wananchi wanaolia kwa kupandikiziwa mtu.
ni jabu la busara kwa kikwete wala sio FAVOR kumteua dr bilal ili kutibu donda kwani bila ya ushirikiano wa pande zote mbili basi ushindi kwa ccm zanzibar utakua ndoto.na ninathubutu kusema Dr bilal ndie aliefanya FAVOR kwa ccm kwa kuridhia kua mgombea mwenza wala sio vice vercer
Inaonyesha jinsi gani hili kundi lilivyo na upeo mdogo wa kufikiri. Msitubabaishe hapa, Kwanza hata kumteua Bilal kuwa running mate wa JK ni favor na politically wise decision, si kwa kuwa ana the best VP qualifications. Ndio maana hakupewa nafasi ya kuongea.
Hongera Dr. Shein na ndugu zangu wanzazibari na wabara tumuunge mkono kwa kuwa ni mwenzetu; wanaopinga mnataka awe rais wa wapi?