
| Kutoka London:Mtutusiko wa 2012 una kiini katika umasikini | Send to a friend |
| Saturday, 14 January 2012 19:48 |
|
NILIKUWA nikiongea na rafiki yangu wa Nigeria akasema kila kukicha Wazungu wanashuka Afrika. “Uchumi wa Ulaya mbaya sana sasa hivi,” ali jamaa huyo huku akicheka; ”si ajabu wanakimbilia Afrika.” Si Wazungu tu, nikamwambia. Wachina wanalikamua bara kama maziwa ng’ombe. Afrika ni tajiri wa madini, mimea, mafuta na wanyama pori. Tovuti maarufu la habari Wikipedia linasema Afrika ina neema kubwa kiasi ambacho pamoja na kuibiwa na wageni na mafisadi wachache, bado hata nusu ya mali asili yake haijagunduliwa au kufaidika sawasawa. Karibuni mafuta yanaendelea kuvumbuliwa na tayari Wachina wanamiliki asilimia 40 ya mali hiyo ya WaSudan mathalan. Wakati huo huo Sudan ni maskini sana. Vita vya wenyewe kwa wenyewe vilipokua vimechachamaa miaka kumi iliyopita ripoti ya Umoja wa Mataifa (HDR) ilieleza asilimia 25 ya Wasudan hawafikishi miaka 40. Sasa hivi tunapoambiwa hali ni mbaya kiuchumi duniani Jumatatu kampuni maarufu ya magari, Rolls Royce, ilitangaza ongezeko la faida kwa asilimia 14 mwaka jana. Wanunuzi wengi wanatoka Marekani na China na wanamudu kununua gari moja kuanzia shilingi 480,000,000 kuendelea. Rolls Royce imeeleza haijawahi kupata faida kiasi hiki tangu ilipoanzishwa miaka 107 iliyopita. Eti kwa vile linazuka tabaka jipya la wenye pesa hasa China. Takwimu za Benki kuu ya Dunia ( mtoa mikopo mkubwa nchi zinazoendelea) zinakiri wanadamu bilioni moja na robo ni maskini wanaoishi kwa mlo mmoja tu kwa siku. Ingawa ulimwengu wetu una wakazi milioni saba, asilimia 80 hutumia pesa wanayoipata kwa chakula, bas. Hii ina maana masuala muhimu kama elimu, afya na makazi hayapatikani. Wengi wanasukuma tu siku. Inanikumbusha msemo wa Kiswahili Bora Twende. Ukitathmini saikolojia yetu Watanzania utagundua baadhi yetu tumo tumo tu. Hatujali kuvaa mikanda katika magari na mabasi (jambo lililodhihirishwa na uchunguzi wa kitaalam duniani kwamba hukinga na kupunguza madhara ya ajali); hatujisomei vitabu au kujiendeleza, hatuangalii afya zetu na unene unazidi kutuletea maradhi kama kisukari na presha ya moyo(hata vijana chini ya miaka 30 wanakumbwa leo). Wiki iliyopita tulitazama neno “tutusa” lenye maana ya kudunda moyo au kutafuta kitu gizani. Tukaona namna mtitiso ulivyoenea duniani kuwa mwaka 2012 ni wa mwisho. Kwamba watabiri wa woga (kama Nancy Lieder, 1995) aliyeanzisha tovuti iitwayo Zeta Talk iliyosema Mei 2003 ungekuwa mwisho na 21 Desemba 2012 ulimwengu wetu utaangamizwa na sayari ya Nibiru Planet X. Ukweli vilio kwamba uhai utakwisha vimetoka mbali sana. Kati ya mwaka 1348 hadi 1350 asilimia 60 ya Wazungu wa bara Ulaya walitokomezwa na tauni. Chimbuko la “kifo cheusi” (Black death) lilianzia miaka 30 awali. Mwaka 1315 dunia ilikumbwa na hali mbaya kimazingira ambapo mavuno na uhaba wa vyakula vilizua njaa, ujambazi, watu “kula watu” wenzao na maradhi. Hatimaye ndipo mapanya yakaenea na msemo wa mwisho wa dunia ukakita; wanajimu wakasema Mungu kakasirika na kadhalika. Wanadamu wanapokosa mambo ya msingi (chakula, malazi na afya) hutafuta majawabu katika kiza na tutusa. Ila unapochunguza, umaskini ndiyo chanzo cha matatizo makubwa ya vita na hasira za wanadamu. Mifano iko mingi Tatizo la vita vya wenyewe kwa wenyewe linaloendelea sasa hivi Somalia na kuwaathiri majirani zetu Kenya limeanzia wapi? Asili mia 95 ya Wasomali wanaishi vijijini. Kati ya wanakijiji hawa walezi wa watoto na familia ni wanawake wasiosoma na ambao hawana haki yeyote katika jamii. Takwimu za Umoja wa Mataifa zimeeleza kiasi cha wanawake 45 wa Kisomali hufa kila siku kutokana na athari za ukeketaji au tohara za akina mama. Vifo hivyo huja nyakati za uzazi unaombatana na damu na maumivu makali. Mbali na mila na desturi kama hizi hali ya hewa imeisambaratisha Somalia. Mwaka 2006 mafuriko makali yalipokumba uwanda wa kati wa nchi yaliendeleza vurugu zilizoanza toka kuangushwa kwa Rais Mohammed Siad Barre, 1991. Labda Somalia ingekuwa na utajiri wa madini mambo yangekuwa afadhali lakini asilimia 60 hutegemea ufugaji. Tatizo hili limezidishwa na ulaji mirungi unaowafanya wanaume kuranda randa ovyo, kutojali mifugo, kazi au familia. Matokeo wananchi 12.4 wameathirika na njaa; milioni 1.5 wako ukimbizini ughaibuni. Nigeria hivyohivyo. Kinyume cha Somalia, Nigeria ni moja wa matajiri Afrika kutokana na mafuta. Mafuta hayo toka majimbo ya kusini (Niger Delta) yamewafanya wananchi wengi walalamike kwamba kipato cha mali hii asilia hakiwafaidi. Mwaka 1995 mwandishi na mtangazaji maarufu wa TV, Ken Saro Wiwa, alinyongwa na serikali kutokana na jitihada zake kupinga uporaji na uharibifu wa mazingira ya watu wa kabila la Ogoni. Ingawa Nigeria ilifukuzwa ndani ya Jumuiya ya Madola kwa miaka mitatu, hali iko vile vile. Asilimia 65 ya Wanigeria ni maskini sana. Tatizo hili limechipusha vyama vyenye itikadi za Kiislamu hasa majimbo ya kaskazini . Kabila la Wahausa na Wafulani (asilimia 30 ya Wanigeria) lina Waislamu zaidi ya Wakristo ambapo kusini wapo Waislamu wachache. Ingawa Uislamu umekuwepo Nigeria toka karne ya 11, miaka 30 iliyopita umechipusha viongozi waliotumia dini hiyo kuleta uhasama kupitia makundi matatu. Boko Haram (“Elimu ya Kizungu ni Dhambi” kwa Kihausa) ilisababisha mauaji ya wananchi 450 mwaka jana. Boko Haram inadaiwa kuwasiliana na magaidi wa Kisomalia. Maitatsine (Kihausa “Yule anayelaani”) iliasisiwa na Mohammed Marwa (aliyefariki 1980) ikipinga baadhi ya nguzo za Kiislamu kama Sunnah na Hadith. Marwa alishutumu “mambo ya Wazungu” mfano redio, baiskeli, magari na pesa. Mwaka 2004 “Maitatsine” ilisababisha vifo 1,000 mjini Yola. Mwaka juzi Darul Islam (“Nchi ya Kiislamu) inayolilia Nigeria iwe ya Waislamu watupu ilisababisha ghasia zilizoua 700. Makundi haya matatu yanalilia Sharia iwe kanuni ya taifa hilo. Ugaidi husababishwa na umaskini; ambao hutokana na siasa na uongozi mbaya. Si ajabu karibuni baadhi ya watabiri wa woga kudai mwisho wa dunia ungekuwa 1994, 1999, 2000, Septemba 2001, Mei 2003, 11 Novemba 2011 na sasa 21 Desemba 2012. Msingi hapa si kuogopa kwisha dunia bali kusuluhisha matatizo ya wale wanaokula mlo mmoja tu kwa siku. Barua pepe: This e-mail address is being protected from spambots. You need JavaScript enabled to view it Tovuti: www.freddymacha.com |

Habari Mpya
Picha
Zenye Mvuto
- Nafasi za Kazi
- Links za wateja na washirika wetu
- Muswada wa madini waitoa jasho serikali
- Bi kizee asafari kilometa 50 kupinga hotuba ya JK, AMUONYA ASITUMIE MADARAKA YAKE VIBAYA
- Mishahara sekta binafsi Tucta yashtukia danganya toto
- Vigogo UVCCM wajiuzulu
- Mwinyi atetea ajira za wafanyakazi, ashauri utu uheshimiwe kudumisha Amani














