|
Kizitto Noya, Bukoba Vijijini
ALIYEKUWA Waziri wa Nishati na Madini, Nazir Karamagi amepata pigo kwenye jimboni lake la Bukoba Vijijini, baada ya wapigakura wake 700 kuhama Chama Cha Mapinduzi (CCM) na kujiunga na Chama cha Wananchi (CUF).
Wapiga kura hao walifikia uamuzi huo baada ya wabunge wa CUF, Habib Mnyaa (Mkanyageni), Shoka Khamis Juma (Micheweni) na Severina Mwijage (viti Maalum) wakiongozwa na Katibu Mkuu wa CUF Seif Hamad kumchambua Karamagi katika mkutano wa hadhara kwa kumhusisha na kashfa ya kampuni ya Richmond.
Katika mkutano huo uliofanyika juzi jioni kwenye viwanja vya kata ya Ibwera, CUF ilichaumbua utendaji wa CCM na kumhusisha Karamagi na matukio ufisadi wa Richmond.
Shoka Khamis Shoka aliwauliza wananchi waliohudhuria mkutano huo sababu za kuendelea kumchagua Karamagi na CCM yake kuwaongoza wakati hajawahi kusema chochote bungeni kuwatetea tangu aingie madarakani mwaka 2003.
"Mimi na Karamagi tulichaguliwa pamoja kwa mara ya kwanza mwaka 2005, tangu niamfahamu bungeni sijasikia hata siku moja akichangia chochote kinachohusu jimbo lake zaidi ya kujitetea mwenyewe kwa kashfa zilizokuwa zikimkabili za Richmond na TICTS," alidai Shoka.
Naye Savelina Mwijage aliwahoji wapigakura hao faida wanayoipa kwa kumchaugia baada ya kupata fulana na kofia za CCM kisha mbunge wao kutoweka mpaka uchaguzi mwingine.
Mbunge huyo ambaye mara nyingi alikuwa anazungumza kwa lugha la Kihaya, aliwataka wakazi wa jimbo kujiunga na chama hicho.
Akizungumza katika mkutano huo Katibu Mkuu wa CUF, Seif Hamad alisema Tanzania inatakiwa kufanya ya uongozi kwa kuwa CCM inachoka, inalewa madaraka na kuanza kuyumba.
Alisema migomo ya vyuo vikuu, walimu na kukithiri kwa vitendo vya ufisadi nchini ni dalili za CCM kushindwa kushughukia matatizo ya wananchi hivyo kutostahili kuendelea kupewa muda kuiongoza nchi.
"Nadhani Watanzania tunatakiwa tufikie mahali tufanye mabadiliko, tuiangalie CCM kwa makini na kutafakari inakopeleka kisha tufanye maamuzi mbadala ya kukiondoa madarakani," alisema
Mkutano huo uliozoa wapigakura wa Karamagi, ilifuatiwa na mikutano kadhaa iliyofanyika katika jimbo la Bukoba Mjini Kwa Naibu wiziri wa Mambo ya ndani Khamis Kagasheki ambako nako Seif aligawa kadi 1900 kwa wanachama wapya wa CUF.
Maalim Seif yuko mkaoni Kagera kwa ziara ya siku kumi ya ujenzi wa chama. Katika ziara hiyo Seif anafungua matawi mapya ya CUF na kusimika viongozi wa matawi na kuwapa maelezo kadhaa ya kujipanga kwa ajili ya uchaguzi wa serikali za mitaa mwakani na Uchaguzi Mkuu wa 2010.
|