MwanzoContactsEmail
Home Uchambuzi Uchambuzi na Maoni Kudhalilika kwa mwanamke kunatokana na mienendo yake
BOOKMARK THIS PAGE
Kudhalilika kwa mwanamke kunatokana na mienendo yake  Send to a friend
Friday, 13 January 2012 10:19

Na Florence Majani
MADA ya wiki  iliyopita iliyozungumzia fedheha wanazozipata wanawake, ilizua mada nyingine nyeti mno.
Kwa baadhi ya waliopiga simu  au kutuma ujumbe mfupi wa maandishi, kwa hakika walionyesha kukerwa na fedheha hizo wanazopata wanawake.

Lakini,  pia wengi wao walikiri kuwa baadhi ya wanawake wenyewe wamekuwa wakichangia katika kudhalilishwa kwao.

Imebainika kuwa, wanawake hali kadhalika ni miongoni mwa wale wanaotumia lugha chafu mno, wakitumia viungo vyao wenyewe kama silaha  unapotokea ugomvi.

Kwa mfano, msomaji Aggrey Nguni wa Morogoro anabainisha kuwa  wanawake mjini hapo ndio vinara wa kutukana tusi lile… linalotaja kiungo cha mzazi mwanamke.

Jambo hili ni la kweli, kwani siku mbili zilizopita nilimshuhudia msichana mmoja akimrushia utingo matusi yale yale yanayotaja viungo vyake mwenyewe baada ya kutokea kutokuelewana baina yao kuhusu nauli.
Wakati unapopigania uhuru wako, usawa na haki, unatakiwa uende sambamba na mazingira ya utetezi wa kile unachokipigania.

Kwa muda mrefu sasa wanawake wamekuwa wakililia haki na usawa. Lakini, je, wamekuwa wakiishi katika mazingira yanayostahili watu kuwapa haki hizo na usawa?

Au, hawazifahamu ni haki gani wanazozililia na wajibu upi wanaopaswa kutenda katika vita hii?

Usawa huu si katika nafasi za viti maalum  bungeni, katika siasa na katika elimu pekee bali ni pamoja na kuhakikisha mwanamke anakuwa chombo cha thamani katika jamii badala ya kugeuka tusi.

Na ili mwanamke awe chombo cha thamani yeye mwenyewe anatakiwa ajithamini kwanza. Ajithamini kwa kutenda maadili yanayokubalika katika jamii.

Anapoutaka usawa, basi asimame katika nafasi ambayo hali halisi ya matendo yake itatoa taswira ya ‘yeye ni nani’ . Ili hata utakapopaza sauti yako, watu wataisikia na kuifanyia kazi.

Kwa mfano, unapovaa mavazi yasiyo na heshima mbele ya jamii, yanayoacha sehemu kubwa ya mwili wako mtupu, unategemea utaheshimika kweli? Ni nani atakuheshimu iwapo wewe mwenyewe hujiheshimu?
 Nani atakuheshimu iwapo mwili wako mwenyewe umeushusha thamani na kuuacha hadharani ili kila mtu, wazee, vijana, watoto wauone au hata kuuchezea?

Kila mtu atakuona una  upungufu fulani na hata inapotokea nafasi katika ofisi yako, watu wataona hustahili nafasi hiyo kwa sababu mavazi yako yanakupa tafsiri mbaya.

Mfano mwingine ni katika bendi zetu za muziki siku hizi, wanaume wanenguaji watavaa mavazi ya kawaida, lakini wanawake watajibana na kuacha robo tatu ya mwili nje.

 Ni lipi linalowanyima nafasi ya kunengua iwapo watavaa mavazi ya kawaida yasiyowaacha watupu?
Tuwaanfalie hata hawa wacheza filamu wetu, endapo atatakiwa balozi  mwanamke wa kuiwakilisha Tanzania, nani atateuliwa miongoni mwa wanawake?

 Thamani ya mtu huanzia kwake (mtu)  mwenyewe, mazungumzo yako, upeo wako, matendo yako, na hata mavazi yako.

Mwanamke mwenyewe unapoibuka na kutukana matusi hadharani ukiainisha kiungo chako mwenyewe,  unategemea nini hasa?

 Unategemea jinsia ya kiume itabadilisha tusi hilo na kuweka kiungo cha kiume? La hasha, hawatabadilisha bali itaendelea kuwa hivyo hivyo.  

Wanawake wenzangu tutaendelea kudhalilika kwa kuwa, hatuko mstari wa mbele kukemea na badala yake tunaongeza mafuta ya taa katika moto uwakao kutokana na baadhi ya matendo yetu.

Napenda kusema kuwa, siwaungi mkono vijana na wengine wanaowashika sehemu nyeti wasichana katika maeneo kama ya masokoni, iwe Buguruni, Ilala, Tandale, Manzese na kadhalika,lakini ni nadra sana kumkuta mwanamke aliyevaa kiheshima -akipigiwa mbinja au kudhalilishwa kwa kushikwashikwa na vijana hawa.

Inasikitisha kuona mwanamke mwenyewe anatoa lugha chafu akihusisha kiungo nyeti cha mwili wake. Jamii itashindwa kumwelewa mtu huyu iwapo ana akili timamu au ana upungufu fulani.

Ni sawa na wale wazazi wanaowatukana watoto wao, ‘mbwa wewe” na wanasahau ya kuwa, kama mtoto ni mbwa, basi hata mzazi ataitwa ‘mama mbwa au baba mbwa’

Iweje mtu achochee mwili wake uwe sehemu ya matukano? Hii ni aibu na kujipalia makaa ya moto vichwani mwetu.

Lakini, tabia hii si kwa wanawake wa mitaani tu, hata baadhi ya waimbaji wetu, ambao walipaswa kuwa kioo cha jamii, mashairi yao yanamchora mwanamke kama mtu mwenye hulka ya kugombania wanaume. Anayezipa baraka ndoa za mitala na kuzipapatikia.

Baadhi ya nyimbo zetu zikiwamo za taarabu naonyesha dhahiri kuwa tunaridhia kuolewa katika mafungu tena kwa kupigana vikumbo.

Kwa mfano siku za hivi karibuni kimezuka kikundi cha ‘kanga moko moko’, wanawake wanafanya matendo ya aibu na kuishusha thamani yao kwa kiasi kikubwa.

Wanacheza katika mtindo ambao unachochea vitendo vya ngono na ni fedheha kubwa kwao wenyewe.

Heshima inaanza na wewe. Pasipo wanawake kujithamini na kujiheshimu hakuna atakayekuheshimu, hata watoto wako nyumbani ukiwa na mienendo ya ajabu ajabu basi nao watapunguza uaminifu kwako.

Kuna wakati fulani mke wa Rais Kikwete, Mama Salma aliwahi kutoa rai hii na kuwaasa wanawake kujithamini.
“Ninyi watoto wa kike!lazima mjitambue kuwa ninyi ni Lulu hamna budi kujilinda ,vaeni mavazi ya heshima ,jilindeni acheni kutoa lulu zenu ovyo,” aliwahi kusema.

Mila zinazomdhalilisha na kumdunisha mwanamke, kama vile, tohara, watoto wa kike kutopelekwa shule, ni mbaya na hatuna budi kuzipiga vita kali.

 Lakini  ukiangalia kwa undani, utawakuta wanawake wamejisahau na kufanya matendo mengine yanayoshusha utu wao.

Laiti kama wanawake wangejua thamani waliyo nayo na wakaitumia vyema basi taifa hili lingeimarika zaidi kupitia wao.

Baadhi ya wanawake waliosimama imara kama Helen Sirleaf Johnson, Rais  wa Liberia, Dk Asha Rose Migiro aliyeko Umoja wa Mataifa kutoka hapa Tanzania, Wangari Maathai (hayati) , mshindi wa tuzo ya Nobel kutoka Kenya, walitambua lulu walizonazo. Walijithamini, wakajiheshimu na wakaitumia elimu yao kuwajibika vyema katika jamii.

 Walitumia nguvu walizojaliwa na Mungu na wakayaleta mapinduzi ya jinsia, uchumi na siasa Afrika.
  Ni jukumu la wanawake kutazama walikotoka, na kupiga moyo konde, kujiheshimu huku wakidhamiria kutenda yaliyo makuu ili wabadilishe mtazamo hasi juu yao.

Hakuna wakulibadilisha hili zaidi ya wanawake wenyewe, endapo watabadilisha mienendo yao.
0715- 773366


Add this page to your favorite Social Bookmarking websites
Reddit! Del.icio.us! Mixx! Free and Open Source Software News Google! Live! Facebook! StumbleUpon! TwitThis Joomla Free PHP
 

Comments 

 
0 #1 2012-01-17 10:01
kwanza kabisa wanawake wajihifadhi katika mavazi yao pia katika lugha zao chafu majumbani mbele za watoto wadogo na hujirahisi kwa wanaume kisa ujila na ujila wenyewe unawezakuta ujila mdogo sana, tofauti na angekaa na akakanda chapati au maandazi au akafungua genge angepata zaidi kuliko kudharirika, tunaomba serikali ya kikwete ikemee mavazi yanayozalilisha wanawake mitaani hata kwenye mavyuo vikuu sikuhizi unakuta kunamavazi ya ajabu sana, suruali imebana kiuno chote kipo nnje. Hasa wanafunzi wa chuo siku hizi wamezidi na hawa wanachuo wa mitaani na wanafunzi wa kawaida naomba serikali ichukue mkondo wake katika kukemea mavazi ya ajabu, maana hata maadili yamepotea kabisa. Unamkuta binti kwenye basi hata kukaa anashindwa kisa nguo inapanda na inamuacha uchi mbele ya baba zao, kaka zao, wajomba zao, mama zao, na watoto wao.
Quote
 

Add comment

Tumia jukwaa ili kutoa maoni ambayo yatasaidia kulijenga taifa letu. Kumbuka, maoni yako yatapitiwa kwanza kabla hayajarushwa hewani!!!!!!


Banner
Banner