IDDA:Mwanamke aliyepania kuwakomboa wanawake

Muktasari:

Anasema katika mdahalo moja ya wadhamini wake walitoa mitaji kwa wanawake 40 iliyowawezesha  kuanzisha biashara za maduka ambayo yanauza vinywaji baridi  katika sehemu mbalimbali za Jiji la Mwanza.

“HAKUNA mtu ambaye anaweza kumsaidia mwanamke na kumuinua kiuchumi kama hajavaa kiatu cha mwanamke huyo na kuona ni njisi gani ameathirika kiuchumi, badala yake wengi huwa wanatumia njia ya mkato kwa kumdharau mwanamke kwa mtazamo wa kuwa hawezi kusimama bila ya kuwa na mwanamume pembeni yake,” hivyo ndivyo anavyoanza simulizi yake Idda Adam.

Idda ambaye ni Mkurugenzi wa Taasisi ya Mikaela, inayuojishughulisha na midahalo ya kumkwamua mwanawake kiuchumi pamoja na kudumisha uhusiano wake katika familia na jamii inayomzunguka, anasema kuwa anaamini mwanamke ni nguzo muhimu katika kukuza uchumi wa familia yake hata katika ngazi ya Taifa.

Anafafanua kwa kusema kuwa, wanaweke wanaofanyiwa ukatili wa kiuchumi ni wale ambao wanatumia nguvu nyingi kushiriki katika kuongeza kipato cha familia, lakini mgawanyo wake katika matumizi unakuwa hauna uwiano na kile alichochangia, baada ya mwanamume kutumia asilimia kubwa ya uchumi huo na kuiacha familia katika hali mbaya ya kiuchumi.

Anasema kuwa, wanawake hao  hapa nchini, wamekuwa wengi na hatimaye wamekuwa wakiathirika na msongo wa mawazo, huku wengine wakikata tamaa ya kushiriki katika kukuza uchumi wa ndani ya familia zao na kuwa watu wa kusubiri kusaidiwa.

Alisema kuwa katika maisha ya makuzi yake, ameshuhudia jinsi ambavyo mwanamke amekuwa akinyayasika katika ngazi ya familia na kuathirika kiuchumi, wakati ni mtu ambaye alichangia kwa kiasi kikubwa katika kukuza uchumi wa familia hiyo.

Anasema kuwa kutokana na hali hiyo, aliishi katika ndoto za kumkwamua mwanamke kiuchumi ikiwemo kutambulika kwa mchango wake katika familia yake.

Alifafanua kuwa, ndoto hizo zilimsukuma kuwakusanya akina mama kuanzia wale walipo katika ngazi ya chini kiuchumi na kuanza kujadiliana jinsi ambavyo wanaweza kujikwamua kiuchumi.

Anasema kuwa katika mijadala hiyo alianza kuona mwanga kwa kuwa wanawake wengi walianza kujiamini na kujiunga katika vikundi vidogo vidogo vya kuweka na kukopa, kisha kuanzisha biashara ndogo ndogo ambazo zimekuwa kiziwaingizia kipato na kuendesha familia zao.

Anasema kuwa kadri siku zilivyokuwa zikienda wazo lake liliendelea kupanuka zaidi na hatimaye akaona aanzishe taasisi ambayo itawakusanya wanawake wengi zaidi na kupata elimu kwa wataamu wa uchumi, mahusiano ya familia, afya pamoja na saikolojia nia ni kumuweka mwanamke katika nafasi nzuri ya kushiriki zaidi katika kukuza uchumi wa familia yake na kumuondolea kovu la kunyanyasika.

Alisema kuwa mwaka 2011 alianza mchakato huo rasmi wa kumkomboa mwanamke na kwa mara ya kwanza, Desemba 2012 alifanya mdahalo wa kwanza ambapo karibu robo ya wanawake walioshiriki katika mdahalo huo, baada ya kupata mafunzo sasa hivi wamekuwa wanawake wenye mafanikio kwani wameanzisha biashara na wengine wameweza kuwa na uhusiano mazuri na familia zao.

Anasema katika mdahalo moja ya wadhamini wake walitoa mitaji kwa wanawake 40 iliyowawezesha  kuanzisha biashara za maduka ambayo yanauza vinywaji baridi  katika sehemu mbalimbali za Jiji la Mwanza.

Anasema kuwa hayo ni mafanikio makubwa kwake kwani lengo kubwa ni kumuinua mwanamke kiuchumi na huo ndiyo mwanzo wa mwanamke huyo kuinuka kiuchumi.

Anasema kuwa kama ilivyo kwa mbuyu,ulianza kama mchicha,hata watu wenye mafanikio  wengi wao walianzia katika hatua za chini mpaka kufikia hapo walipo na siri kubwa nyuma yao ilikuwa ni juhudi walizokuwa nazo katika kutafuta.

Anasema kuwa ana amini kuwa mdahaloro wa pili ambao utafanyika Machi  mwaka huu, utakuwa na mafanikio makubwa kuliko ule wa kwanza, kwa sababu washiriki wake watatoka kuanzia vijiji hadi mijini, hivyo kuwafanya wanawake wengi kupata elimu ambayo itamfanya kujikwamua katika hali mbaya ya kiuchumi.

Anasema kuwa katika mdahalo wa mwaka huu kauli mbiu yake yake itakuwa,’ Mwanamke katika Njia ya Kuelekea katika mafanikio’  na itazungumziwa kwa udani zaidi ya ile ya mwaka jana.

Anasema kuwa kutakuwapo na mwezeshaji ambaye amebobea katika mambo  ya uhusiano ambayo yatamfaya mama kuwa na uhusiano mzuri baina yake na watoto wake, tofauti na hivi sasa wanawake ambao wamepata bahati ya kufanya biashara au kazi, wamekuwa wakiwaachia watoto wao kulelewa na dada wa kazi na wakati mwingine majukumu ya malezi kuachiwa walimu mashuleni kwao.

Anasema kuwa inakuwa haina maana ya mama kutafuta fedha halafu zinashindwa kutumika katika maana nzuri, kwa sababu watoto wanakuwa wamelelewa katika malezi ambayo hayana msingi na hatimaye muda wote familia inaishia katika mifarakano.

Aliongeza  kuwa  mwanamke ambaye anachangia ukuaji wa uchumi katika familia yako haina maana asiwe na uhusiano mazuri ya kindoa na mume wake la hasha, wanawake wanatakiwa kuweka uwiano wa maisha yao ya kiuchumi na familia.

Anabainisha kuwa, mwanamke anatakiwa kuwa na mahusano mazuri na jamii yake inayomzuka anatakiwa kushiriki shughuli zote za kijamii.Katika upande wa afya alisema kuwa watakuwa na kipengele kimoja cha kupunguza kasi ya maambukizo ya HIV pamoja na unyanyapaa kwa wale ambao wameisha ambukizwa, alisema kuwa sio kuwa mwanamke aliyepata maambukizo hawezi kuchangia kukuza kipato cha familia kuwa wanaweza na wapo ambao tayari wameisha kuwa mfano bora katika jamii.

Anasema wanawake wanatakiwa kuwa mstari wa mbele kupinga unyanyapaa kwa wale ambao wamepata maambukizo na kudai kuwa wao wakifanya hivyo, unyanyapaa utaisha na kila mtu anakuwa na msaada kwa waathirika.

Anasema kuwa mama ndiyo nguzo ya familia kwa maana nyingine, basi hata katika kuongeza kipato katika familia anatakiwa pia kuwa nguzo muhimu hivyo mada ya ujasiriamali,uwekezaji itakuwa mada ambayo itaongelewa kwa mapana zaidi na wataalamu mbalimbali ambao watakuwa wameandaliwa.

Anasema kuwa baada ya kupata mafunzo hayo ana imani kuwa, kila mwanamke atakuwa na mawazo mapya, fikra mpya na mwanzo wa kuwa mwanamke ambaye atakuwa na mchango mkubwa katika familia yake.

Idda anasema kuwa wanawake wanatakiwa kujiamini na kuamini kile wanachofanya katika uhuru binafsi wa maisha na wanatakiwa kuhakikisha wanafanikiwa kwa kile wanacho kiamini kuwa ni moja nguzo ya mafanikio yao.