Hii ya Kamati ya Saa 72 inatengeneza maswali

Muktasari:

  • Mashindano hayo yaliyofana mwaka huu, yamemalizika juzi usiku kwenye Uwanja wa Amaan kwa Azam kutwaa ubingwa kwa kuilaza URA kwa mikwaju ya penalti 5-3.

        L igi Kuu Tanzania Bara inaanza mikikimikiki yake baada ya kusimama kupisha Kombe la Mapinduzi.

Mashindano hayo yaliyofana mwaka huu, yamemalizika juzi usiku kwenye Uwanja wa Amaan kwa Azam kutwaa ubingwa kwa kuilaza URA kwa mikwaju ya penalti 5-3.

Lengo si kuyajadili mashindano hayo, lakini kikubwa ni kutaka kuangalia yaliyotukia hivi karibuni kwa TFF.

Ligi ikiwa imesimama, tulielezwa kuwa kuna baadhi ya matukio ambayo yalijiri tangu ligi hiyo ilipoanza Agosti mwaka jana ikiwamo vitendo vya utovu wa nidhamu ambao umekuwa ukizigharimu timu pamoja na wachezaji, makocha na viongozi wa klabu.

Kwanza inashangaza kuona matukio haya kujirudiarudia, lakini pengine ni kutokana na presha za mechi husika.

Nataka kuiangalia Kamati ya Saa 72 ya Shirikisho la Soka Tanzania, TFF, ambayo kwa sehemu kubwa ndiyo wasimamizi wa ligi.

Kamati hiyo ndiyo inayotoa adhabu mbalimbali kwa klabu, makocha na wachezaji. Juzi hapa naweza kusema ilitoa mpya kwa kutoa adhabu kwa wachezaji, viongozi na timu, sasa shangaa ni kutokana na makosa yaliyofanyika muda mrefu, tofauti na ilivyokuwa inatarajiwa.

Iliziadhibu Mbao FC na kocha wao, Etienne Ndayiragije na wachezaji kadhaa wa timu mbalimbali akiwamo Obery Chirwa wa Yanga na Lambert Sabyanka wa Prisons kwa kuwasimamisha ama kupiga faini.

Kama nilivyosema kuwa inashangaza hali hii na pengine ni kutokana na tensheni ya mechi zao na ni wazi inadhihirisha kuwa kuna shida ya utovu wa nidhamu katika Ligi Kuu.

Ninachokiona hapa, si kwa timu hii, kuna tatizo la kinidhamu. Kwa mchezaji, kocha au viongozi, nidhamu ni msingi wa kila jambo .

Hata wachezaji wa soka kucheza bila ya nidhamu ni jambo linalowakwanza kufika mbali.

Inafahamika kwamba, klabu zisizo na nidhamu ni vigumu kufikia mafanikio ambayo wengi wanatamani kufika huko wanakokimbilia.

Nidhamu mbovu uharibu ladha ya mchezo kwa sababu inaweza kutokea kocha kufungiwa, kusimamishwa kitaifa ama kimataifa.

Klabu zinatakiwa kufahamu kuwa Ligi Kuu pamoja na wachezaji wote, makocha na hata viongozi wake kuwa ni vyema kujikita katika nidhamu, ili waweze kufika mbali na kusaidia kuinua soka letu.

Wakati mwingine, inawezekana TFF inashindwa kukemea suala hili kwa vile yenyewe inanufaika kwa faini inazozipiga timu, wachezaji, makocha na viongozi na kutunisha mifuko ya shirikisho hilo, lakini nidhamu mbovu ina athari kubwa kwa soka letu.

Hata kama suala la nidhamu nzuri ama mbovu ni suala linalomhusu mtu mmoja, lakini viongozi na makocha wanawajibu mkubwa wa kuwasaidia wachezaji wao kwa kuwaonya mapema na kuwataka kuingia viwanjani wakiwa na utulivu wa akili.

Kama kocha wa timu hana nidhamu wala kuwa na uwezo wa kuhimili presha za uwanjani na kufanya matendo ya ovyo na utovu wa nidhamu, ni vipi ataweza kuwahimili wachezaji wake. Kiongozi asiyeweza kuhimili vishindo vya uwanjani atawezaje kuanza kuwatuliza wachezaji wake pale wanapokuwa na munkari?

Cha msingi ni wachezaji kutofanya mambo yanayokwenda kinyume na soka lakini zaidi kwa TFF kutangaza adhabu kwa wakati.

Inapendeza kama mchezaji, kocha au timu akiadhibiwa palepale inapotokea amefanya makosa kuliko sasa kunaweza kuonekana kama dili kwa kuwafungia wachezaji muhimu baada ya kuona mchezo fulani unaelekea au unakaribia.