Issa Juma anavyozitamani ligi za barani Ulaya

Muktasari:

  • Kiungo huyo aliitwa kwenye ule mchezo wa kirafiki dhidi ya Malawi na kocha wa Taifa Stars, Salum Mayanga ili kuziba nafasi ya Orgeness Mollel wa FC Famalicao ya Ureno ambaye alishindwa kuwasili

Mtibwa Sugar inajivunia kiungo wake, Issa Juma ambaye licha ya kucheza eneo la kiungo wa kati pia ana uwezo wa kucheza nyuma ya mshambuliaji (10) na hata kwenye eneo la ushambuliaji wa mwisho.

Kiungo huyo aliitwa kwenye ule mchezo wa kirafiki dhidi ya Malawi na kocha wa Taifa Stars, Salum Mayanga ili kuziba nafasi ya Orgeness Mollel wa FC Famalicao ya Ureno ambaye alishindwa kuwasili.

Issa mwenye asili ya Zanzibar amezungumza na Spoti Mikiki na kuelezea mambo kadhaa ambayo wadau wengi wa soka hawafahamu kuhusu yeye hasa alipoanzia kucheza soka na tabia yake kwa ujumla.

“Kuna timu moja ya mtaani inaitwa Jamaica ya Zanzibar hiyo ndiyo nilianza kuichezea wakati nikiwa mdogo, 2010 hadi 2013 na ndipo nilipoanza sasa kuangaikia kwa kutafuta timu kubwa ya kuichezea,” anasema Issa.

Changamoto

“Nimepitia mengi sana lakini kikubwa ni changamoto ya kutokuwa na jina kubwa, ilinifanya kuwa na wakati mgumu sana, hakuna aliyekuwa anajali kuhusu mimi mpaka pale atakaponiona nacheza. “Mtibwa nilifanya majaribio na kufuzu ila ilibidi kuanza kuonyesha kwa nguvu zote ili nianze kujijengea jina, kwa kiasi chake nimefanikiwa, ukiwa haufahamiki ningumu sana kwenda sehemu na kupata nafasi moja kwa moja,” anasema.

Mavazi

“Sio mtu wa mambo mengi kwenye mawazi, mara kwa mara navaa tisheti na jinzi ila sio kwamba ndiyo nguo ninazo zipenda, huwa napenda sana kuvaa suti ila tatizo lile ni vazi ambalo huwezi kulivaa kila wakati,” anasema Issa.

Malengo

“Wachezaji wengi wa hapa nyumbani maisha yao ya mpira huishia Yanga na Simba, sipendi na kwangu iwe hivyo natamani sana kama nitashindwa kufika Ulaya basi nicheze hata Ligi ya Afrika Kusini,” anasema Issa.