Kane utampenda, apiga bao la maana Arsenal ikifa Wembley

Muktasari:

Mauricio Pochettino, amesema hakuna mshambuliaji mahiri kama Harry Kane.

Mauricio Pochettino, amesema hakuna mshambuliaji mahiri kama Harry Kane.

Kocha huyo amemtaja Kane ni mmoja wa washambuliaji hodari aliyewahi kumuona duniani.

Kauli ya kocha huyo imekuja muda mfupi, baada ya Kane kufunga bao maridadi la mpira wa kichwa dhidi ya Arsenal juzi usiku.

Tottenham Hotspurs ikiwa nyumbani kwenye Uwanja wa Wembley, ilishinda bao 1-0, katika mchezo wa Ligi Kuu England.

Spurs inatumia uwanja huo kwa kuwa White Hart Lane upo katika matengenezo makubwa.

Mshambuliaji huyo wa timu ya Taifa ya England, aliruka hewani baada ya kumzidi maarifa nahodha wa Arsenal, Laurent Koscielny kabla ya kumtungua kipa Petr Cech dakika ya 49.

Matokeo hayo yameisogeza Spurs hadi nafasi ya tatu katika msimamo wa Ligi Kuu England nyuma ya Manchester City na Manchester United.

Man City imezidi kujikita kileleni baada ya juzi usiku kuvuna pointi tatu kwa kuilaza Leicester City ikiwa nyumbani kwenye Uwanja wa Etihad.

Kocha wa Arsenal, Arsene Wenger amekubali bao la nahodha huyo wa timu ya Taifa ya England.

Wenger alisema mshambuliaji huyo alicheza kwa kiwango bora katika mchezo huo.

“Wakati mwingine inabidi ukubali kwa sababu ya kazi nzuri anayofanya. Lakini nataka nikwambie, narudia kwa uzoefu wangu ni mmoja wa wachezaji mahiri duniani,” alisema Pochettino.

Alisema Kane ni hazina ya sasa na baadaye kwa kuwa ana kipaji cha soka ambacho kimekuwa chachu ya mafanikio Spurs.

Kocha huyo raia wa Argentina, alisema anajivunia kuwa na mshambuliaji aina ya Kane ambaye ana uwezo mzuri wa kufunga mabao akiwa katika nafasi yoyote uwanjani.

“Kane ni mshambuliaji wa aina yake. Anafunga dhidi ya beki yeyote anayecheza naye,” alisema Pochettino.

Mshambuliaji huyo alisema ni faraja kwake kufunga bao katika mchezo mgumu uliokuwa na ushindani.

Bao la Kane linaweza kuzidisha shauku ya kocha wa Real Madrid, Zinedine Zidane ambaye amekuwa akimmezea mate muda mrefu.

Real Madrid iliwahi kumtupia ndoano Kane katika usajili wa dirisha dogo kabla ya mpango huo kukwama. Zidane anasubiri usajili wa majira ya kiangazi.