Wametisha kombe la Mapinduzi

Muktasari:

  • Zamu ya makocha kuumiza vichwa, kuwatumia ama kuwaacha waendelea kusugua benchi

Kombe la Mapinduzi limemalizika mwisho wa wiki hii na kushuhudia baadhi ya wachezaji kutoka Azam, Simba na Yanga ambao hawapati nafasi za mara kwa mara kucheza kwenye ligi lakini kwenye mashindano hayo walitakata.

Kutakata kwa wachezaji hao kunaleta ugumu kwa makocha kufanya uamuzi katika upangaji wa vikosi kutokana na viwango bora vilivyoonyeshwa wao ambao si machaguo yao ya kwanza.

Makocha wa timu za Azam, Simba, Yanga na Singida United zinashiriki Ligi Kuu Tanzania Bara, kwa upande mwingine huenda wakalazimika kupangua vikosi vyao vya kwanza ambavyo vimezoeleka ili kutoa nafasi kwa baadhi ya wachezaji waliofanya vizuri kwenye mashindano hayo.

Spoti Mikiki linakuletea wachezaji ambao wametamba katika michuano hiyo ambao kwenye ligi nafasi zao za kucheza ni finyu.

Jamal Mwambeleko, Simba

Katika mechi ya kwanza Simba dhidi ya Mwenge iliyomalizika kwa sare ya kufungana bao 1-1, bao la Simba lilifungwa na Mwambeleko kipindi cha kwanza tena dakika ya pili lakini timu yake haikufika mbali kwenye mashindano hayo walitolewa katika hatua ya makundi.

Mwambeleko aliyesajiliwa kutoka Mbao FC, licha ya kufanya vizuri kwenye mashindano hayo lakini nafasi yake ya kucheza katika ligi anabanwa na Erasto Nyoni au Mohammed Hussein ‘Tshabalala ‘.

Ramadhani Kabwili, Yanga

Kipa wa Yanga ambaye amesajiliwa na timu hiyo kwa mkataba wa miaka mitano akitokea katika kikosi cha Serengeti Boys anaweza kuonesha kiwango katika mashindano hayo ya Mapinduzi.

Kabwili amecheza mechi mbili za makundi na kufungwa bao moja huku mechi zote Yanga ikiibuka na ushindi lakini licha ya kucheza vizuri katika mashindano hayo, hapati nafasi ya kucheza kwenye ligi

Mwinyi Kazimoto, Simba

Kiungo mkongwe wa Simba ambaye alionyesha kiwango safi katika mechi ya kwanza ya makundi dhidi ya Mwenge na kuchaguliwa kuwa mchezaji bora wa mechi na alizawadiwa king’amuzi cha Azam.

Kazimoto ambaye ni fundi katika kuuchezea mpira, anastahili pongezi kwa kazi ambayo waliofanya lakini ni miongoni mwa wachezaji ambao wanakosa nafasi ya kucheza katika kikosi cha Simba ambacho kinaongoza msimamo wa Ligi Kuu Bara.

Haji Mwinyi, Yanga

Aameonyesha kiwango bora kwenye mashindano ya Chalenji yaliyofanyika Kenya mwishoni mwa mwaka jana na mashindano ya Kombe la Mapinduzi.

Kiwango chake ni kama salamu kwa Gadiel Michael ambaye ndiye aliyempoka namba. Uamuzi ni wa Lwandamina.

Moses Kitandu, Simba

Mshambuliaji wa Simba ambaye anacheza mechi zote nne za hatua ya makundi na kufunga goli moja katika mechi dhidi ya Jamhuri na kushinda 3-1.

Kitandu katika ligi hapati kabisa nafasi ya kucheza kwani nafasi yake kuna wakongwe John Bocco na Emmanuel Okwi ambaye anaongoza katika msimamo wa wafungaji wa Ligi Kuu akiwa ameshafunga magoli nane.

Peter Paul, JKU

Mpaka hatua ya makundi inakamilika alikuwa ameshafunga magoli matatu na kuwa katika vinara wanaongoza kufunga kwenye mashindano hayo akiwa sambamba na Ahmad Halika wa JKU.

Paul nafasi yake katika ligi ni ndogo, kwenye Kombe la Mapinduzi amefunga goli moja katika mechi chache alizocheza na licha ya kuingia katika muda wa nyongeza.

Maka Edward, Yanga

Kiungo fundi wa Yanga ambaye alimpandisha katika ligi kuu akitokea katika timu yao ya vijana amecheza mechi mbili za mwisho za Makundi ambazo walicheza dhidi ya Zimamoto na Singida United.

Maka alicheza katika Mapinduzi lakini kwenye ligi hajacheza hata mechi moja kwani nafasi yake huwa anacheza Raphael Daud na Kabamba Tshishimbi.

Emmanuel Mseja, Simba

Kipa ambaye wakicheza hata mechi moja katika ligi kutokana na nafasi yake kucheza kipa namba moja Tanzania Aishi Manula lakini katika mashindano hayo amecheza mechi zote.

Mseja hakuonyesha kiwango kizuri kwani katika mechi nne ambazo Simba wamecheza katika hatua ya makundi amefungwa magoli manne na pengine ni kutokana na kuzongwa na benchi tofauti na vile angekuwa anapangwa.

Mwidini Ali, Azam

Kipa mkongwe wa Azam yupo katika kikosi hiko kwa muda mrefu na alipata nafasi ya kucheza kwenye mechi kadhaa ingawa katika ligi hapati nafasi hiyo.

Azam katika ligi humtumia kipa wao mahiri, Razack Abarola ambaye hata katika mashindano hayo alitamba kwa kudaka vizuri mechi chache tu alizocheza dhidi ya Simba na Singida United.

Pato Ngonyani, Yanga

Beki wa kati wa Yanga ambaye kwenye ligi hana nafasi kabisa ya kucheza kutokana na nafasi yake kuzibwa na Kelvin Yondan na Vincent Andrew ‘Dante ‘.

Pato amecheza mechi mbili katika hatua ya makundi kama kiungo mkabaji na kuingia katika wachezaji ambao hawapati nafasi ya kucheza kwenye kwenye ligi kuu ambayo itaendekea mwisho wa wiki hii.

Salum Kipaga, Singida

Mtihani kama huo unamkabili kocha wa Singida United, Hans Van der Pluijm atalazimika kumpanga Mudathir Yahya au Salum Kipaga kwenye nafasi ya kiungo mkabaji.

Mudathir alikuwa lulu kwenye Ligi Kuu na Mashindano ya Chalenji yaliyofanyika Kenya mwaka jana lakini, Kipaga ametumia vyema fursa ya Kombe la Mapinduzi kujitangaza. Ameonyesha soka ya hali ya juu.

Said Makapu, Yanga

Kiungo mkabaji wa Yanga amecheza mechi zote katika mashindano hayo na katika mechi za mwanzo alikuwa akicheza kama kiungo mkabaji lakini alikuja kubadilishia namba.

Makapu amemaliza mechi tatu za mwisho katika hatua ya makundi akicheza kama beki wa kati baada ya Abdallah Shaibu na Kelvin Yondan kuumia na kuchaguliwa kuwa mchezaji bora wa mechi ya nusu fainali dhidi ya URA.

Matheo Anthony, Yanga

Straika wa Yanga ambaye alisajili misimu miwili iliyopita na Yanga baada ya kuonekana katika mashindano hayo ya mapinduzi amepewa nafasi ya kucheza safari hii.

Anthony kwenye ligi hajacheza hata mechi moja kwani nafasi yake huwa wanacheza Ajibu, Amiss Tambwe, Donald Ngoma na Obrey Chirwa ambao ambao ndio hupewa nafasi ya kucheza mara kwa mara.

Juma Mahadhi, Yanga

Winga wa Yanga mpaka mashindano yanamalizika alikiwa amefunga magoli mawili dhidi ya Mlandege katika mechi ya kwanza dhidi katika hatua ya makundi.

Mahadhi amecheza mechi nyingine nne hadi walipotolewa katoka hatua ya nusu fainali na URA lakini kwenye ligi nafasi yake ni ndogo na huishia benchi.

Said Mussa, Yanga

Winga machachari wa Yanga ambaye walimpandisha akitokea katika timu ya vijana msimu huu baada ya kufanya vizuri kwenye kikosi cha Serengeti Boys amecheza mechi mbili za hatua ya makundi ingawa alikuja kuumia katika mechi ya mwisho.

Said hata katika wachezaji wa akiba wa Yanga kwenye ligi huwa akai lakini huku aliweza kupewa nafasi na kucheza.

Brayson Raphael, Azam

Kiungo wa Azam hana nafasi ya kucheza kabisa kwenye kikosi hicho katika mechi za ligi lakini amecheza vizuri katika mashindano ya Mapinduzi.

Raphael hupanda na kwa uwezo alionyesha katika mashindano hayo anapewa nafasi ya kucheza kwenye ligi kwani anastahili kuwepo katika wachezaji wa Azam ambao wanacheza kwenye ligi.

Yusuph Mhilu, Yanga

Winga wa Yanga alipandishwa na timu hiyo akitokea katika kikosi chao cha vijana na alikuwa akipata nafasi mara chache za kucheza na zikiwa zimebaki dakika za majeruhi japo soka yake inaonekana kuwa ya kiwango.

Mhilu amekuwa mchezaji wa kucheza mwanzo mwisho kwenye mashindano hayo akishirikiana na Ibrahim Ajib katika safu ya ushambuliaji.