Chirwa aahidi kuvunja ngome za Simba, Yanga

Muktasari:

Chirwa ni mchezaji aliyeichezea Yanga kwa mafanikio makubwa na kufanikiwa kuisaidia timu hiyo kutwaa mataji mawili mfululizo sasa ameungana na Azam FC na kuuahidi makubwa.

MSHAMBULIAJI wa zamani wa Yanga, Obrey Chirwa ameahidi neema ya mabao katika klabu yake mpya ya Azam FC mara baada ya kusaini mkataba wa mwaka mmoja kuitumikia klabu hiyo.

Chirwa amejiunga na Azam FC akitokea Misri ambapo alikuwa anakipiga katika klabu ya No-goom El Mostakbal Football Club ambapo ameshindwa kuendelea kutumikia mkataba wake kutokana na kushindwa kumlipa mishahara yake ya miezi mitatu.

Akizungunmza Dar es Salaam jana mara baada ya kutambulishwa na klabu hiyo Chirwa alisema amejiunga Azam kwaajili ya kazi moja tu kuisaidia timu hiyo kutwaa ubingwa msimu huu.

Alisema kazi yake uwanjani kutokana na nafasi anayocheza ni kupachika mabao tu hivyo anampango wa kufunga zaidi ya mabao kumi hadi msimu utakapoisha huku akiweka wazi kuwa katika idadi hiyo ya mabao lazima afunge 'hat- trick'.

"Nimejiunga Azam sio kwamba ni kwaajili ya kumaliza soka lanu ni kama njia tu kwani ninampango wa kutoka tena kwenda kujaribu soka la kulipwa nje ya Tanzania," alisema Chirwa.
Chirwa ametua Azam huku ligi hiyo ikitarajiwa kwenda mapumzikoni kupisha maandalizi ya mechi za kimataifa za kufuzu mashindano AFCON.

Hadi sasa Azam inaongoza msimamo wa Ligi Kuu ikiwa imekusanya alama 30 huku vigogo Simba na Yanga kwenye nafasi ya pili na tatu wakiwa na pointi 26 kila moja wakitiofautiana mabao.