Mkwasa apangua kikosi cha Zahera

Muktasari:

  •  Yanga wanashuka dimbani kumenyana na Ndanda ukiwa ni mchezo wao wa tano wa Ligi wanashuka dimbani wakiwa na kumbukumbu mbaya ya kupoteza nafasi ya kuwania nafasi ya makundi Kombe la Shirikisho.

KOCHA Charles Mkwasa amekipangua kikosi kilichokuwa kikitumiwa na mtangulizi wake, Mwinyi Zahera akifanya mabadiliko kadhaa huku, Sadney Urikhob na Juma Balinya wakikosekana kabisa kwenye kikosi kinachojiandaa kuifaa Ndanda Fc jioni hii.
Hata hivyo Mkwasa anayekaimu Ukocha Mkuu kwa sasa kwa muda Jangwani amemuanzisha Patrick Sibomana kwenye kikosi dhidi ya Ndanda, huku Jaffar Mohammed na Rafael Daud wakianza licha ya enzi za Zahera walikuwa hawapo kikosi cha kwanza cha Vijana wa Zahera..
Yanga inajiandaa kushuka kwenye Uwanja wa Nangwanda Sijaona mjini Mtwara wakiwa wageni wa Ndanda, huku ikiwa na kumbukumbu ya kushinda mchezo wake wa mwisho wa ligi dhidi ya Mbao FC ugenini.
Kwa mujibu wa kikosi kilichotolewa na mtandao wa klabu hiyo mkwasa amewarudisha kikosini Raphael Daud, Jaffary Mohammed ambao walikuwa hawana namba kwenye kikosi cha kwanza cha Zahera.
Mbali na nyota hao waliopewa nafasi wachezaji wengine wanaotarajia kuanza kwenye mchezo huo ni Farouk Shikhalo, Juma Abdul, Kelvin Yondani, Ally Mtoni, Papy Tshishimbi, Deus Kaseke, Mapinduzi Balama na David Molinga.
Issa Bigirimana aliyekuwa majeruhi ameingizwa kikosini akianzia benchi, huku Sadney Urikhob aliyekuwa hakosekani kikosi cha kwanza akiwa hayupo kama Balinya aliyeshindwa kuambatana na timu mjini humo.


GSM WAENDELEZA BONASI
Yanga washindwe wao tu hivyo ndio unaweza kusema mara baada ya wadhamini wao GSM kuendelea kuweka kitita chao cha Million 10 mezani kwaajili ya mchezo wao huo.
GSM inautaratibu wa kuweka fedha hizo kwaajili ya motisha kwa nyota wao na leo wameiweka mezani tayari endapo Yanga itaibuka na ushindi basi wachezaji wao wataoga noti.