Namungo FC yawafungulia milango Kikoti, Lusajo

Dar es Salaam. Uongozi wa Namungo FC umewasha taa ya kijani kwa wachezaji wake kujiunga na timu nyingine huku ikitaka kufuatwa kwa taratibu badala ya kufanya makubaliano kiholela.

Tamko hilo la Namungo FC limetolewa siku chache baada ya kuibuka kwa taarifa za kundi kubwa la mastaa wake kuwaniwa na timu za Simba, Yanga na Azam FC.

Wachezaji wanaowaniwa ni Hashim Manyanya, Lucas Kikoti, Miza Christom, Blaise Bigirimana na nahodha Reliants Lusajo.

Mwenyekiti wa Namungo FC, Hassan Zidadu ameiambia Mwananchi jana kuwa, “hizo taarifa tunazisikia lakini hadi sasa hakuna ofa iliyokuja rasmi. Wachezaji wote hao wanaotajwa wana mikataba na Namungo na suala la kuwaongezea mipya ndio liko mezani. Lakini hata kama wana mikataba, tunafahamu kwamba hatuwezi kumlazimisha mchezaji kubakia kama hana nia na ni vigumu kumzuia kwenda timu nyingine ikiwa ataamua hivyo, inawezekana ni fursa kwake kupiga hatua.

Hata hivyo, Kocha wa Namungo FC, Hitimana Thiery alisema jana kuwa ameuomba uongozi kuhakikisha nyota wake tegemeo wanabaki ili waendelee kuwa na timu yenye ushindani msimu ujao.

“Mimi binafsi sina mamlaka ya kusajili zaidi ya kupendekeza na wenye jukumu hilo ni viongozi wa timu. Kuhusu hao wachezaji nimeshawajulisha na wameshaanza kulifanyia kazi hilo,” alisema.

Ikiwa wataondoka, itakuwa ni muendelezo wa klabu za Simba, Yanga na Azam kuzibomoa timu ambazo zinaibuka na kufanya vizuri katika msimu mmoja wa ligi. Mara baada ya Mbeya City kutamba katika misimu yake miwili ya mwanzoni katika Ligi Kuu, kikosi chake kilibomolewa baada ya Deus Kaseke, Rafael Daud na Peter Mwalyanzi kusajiliwa na klabu hizo.

Ni kama ilivyotokea kwa Mbao FC ambayo baada ya kushiriki Ligi Kuu kwa mara ya kwanza msimu wa 2016/2017, zaidi ya nyota sita waliondoka na kujiunga na klabu hizo. Hao ni Pius Buswita, Emmanuel Mseja, Jamal Mwambeleko, Emmanuel Mseja na Salmin Hozza.