Pepe ageuka lulu Arsenal

Muktasari:

  • Winga wa Arsenal Nicolas Pepe amesifiwa kwa kiwango bora alichokionyesha katika mchezo ambao Arsenal ilishinda mabao 4-0 dhidi ya Newcastle United.

London, England. Graeme Souness amesifu kiwango bora cha winga wa Arsenal Nicolas Pepe katika mchezo dhidi ya Newcastle United.

Kauli ya mchambuzi huyo imekuja muda mfupi baada ya Pepe kutangazwa mchezaji bora katika mchezo huo ambao alifunga bao.

Pepe alicheza kwa kiwango bora na kuchangia matokeo mazuri ya mabao 4-0 iliyopata Arsenal jana kwenye Uwanja wa Etihad.

Souness alisema Pepe aliyefunga mabao manne tangu alipotua Emirates atakuwa mchezaji nyota kama nahodha wa zamani wa timu hiyo Thierry Henry.

Alisema Henry hakuanza vizuri alipojiunga Arsenal, lakini baadaye alikuwa ndiye mfungaji bora wa timu hiyo katika mashindano yote.

Pepe alipata wakati mgumu baada ya kuzomewa mara kwa  mara na mashabiki wa klabu hiyo ambao waliponda kiwango chake licha ya kununuliwa kwa Pauni72 milioni akitokea Lille ya Ufaransa.

“Nadhani ni mchezaji bora, bora zaidi. Utaona Thierry Henry hakuanza vizuri msimu wa kwanza, ilimchukua muda na akawa mchezaji bora, naona pia kwa Pepe atakuwa mchezaji nyota,” alisema kiungo huyo wa zamani wa Liverpool.

Wakati huo huo, kocha wa zamani wa Newcastle Chris Hughton pia amesifu kiwango bora cha Pepe akimtaja kuwa ni mchezaji mwenye kiwango bora.