#WC2018: Watoto wa pangoni waikosa fainali Ufaransa, Croatia

Muktasari:

  • Licha ya watoto hao na kocha wao kupewa mwaliko na Shirikisho la soka la kimataifa (Fifa) kuhudhuria mchezo wa fainali ya Kombe la Dunia 2018, hawataweza kuhudhuria mechi hiyo itakayowakutanisha Ufaransa na Croatia hapo Jumapili.

Moscow, Russia. Unawakumbuka wale watoto wanasoka chipukizi wa Thailand waliokwama pangoni kwa zaidi ya wiki mbili na kuihangaisha Dunia kusaka mbinu za kuwatoa pangoni?.

Licha ya watoto hao na kocha wao kupewa mwaliko na Shirikisho la soka la kimataifa (Fifa) kuhudhuria mchezo wa fainali ya Kombe la Dunia 2018, hawataweza kuhudhuria mechi hiyo itakayowakutanisha Ufaransa na Croatia hapo Jumapili.

Hiyo inatokana na madaktari wanaowatibu watoto hao kusema watahitajika kuendelea kuwa chini ya uangailizi wa kitabibu kwa wiki mbili zaidi kutokana na kupigwa na baridi kwa kipindi kirefu na upungufu wa maji mwilini.

Ili kuwaokoa wanasoka hao chipukizi, jumla ya oporesheni tatu za kimataifa zilizohusisha wazamiaji bingwa zaidi ya 50 kutoka mataifa mbalimbali duniani zilifanyika, lakini zikasababisha kifo cha mzamiaji mmoja raia wa Thailand.

Fifa haijasema chochote baada ya taarifa hizo za watoto hao kukosa fursa ya kuhudhuria mchezo huo wa fainakli kama wageni maalum wa Fifa.