Cannavaro: Sina shaka na Yanga kimataifa

Muktasari:

  • Kiongozi Yanga amedai kikosi hicho kina uzoefu na mashindano ya kimataifa ambapo alisema hana shaka kabisa kwamba msimu huu watafanya maajabu.

Dar es Salaam. Meneja wa Yanga, Nadir Haroub 'Cannavaro' amesema uhodari waliouonyesha mastaa wa kikosi hicho katika msimu ulioisha anaamini moto huo utaendelezwa katika mashindano ya kimataifa.

Cannavaro alisema Yanga imepata nafasi ya kipekee na wachezaji walikuwa wana hamu kuona wanashiriki michuano ya kimataifa, jambo linalomuaminisha wataonyesha makubwa kimataifa.

"Kitu ukiwa na hamu nacho unakipokea kwa thamani kubwa, hilo naliamini kwa wachezaji wa Yanga ambao walipambana kwa kadri walivyoweza kwenye Ligi Kuu Bara na kumaliza nafasi ya pili licha ya kupitia ukata.

"Yanga ni klabu kubwa nchini, ina uzoefu wa kufanya vyema kimataifa, sina shaka na ushiriki wetu kwa mwaka huu, tutafanya makubwa dhidi ya timu pinzani.

"Kupita usajili ambao viongozi wanafanya utaongeza nguvu wachezaji waliopo kuwa na kikosi imara chenye ushindani dhidi kuanzia ligi kuu mpaka klabu ya mabingwa," alisema Cannavaro.