Azam FC yamtambulisha Cioaba rasmi, Ndayiragije atimka

Muktasari:

  • Cioaba aliondoka Azam 2018, baada ya kushindwa kukubaliana na viongozi wa klabu hiyo kutokana na mfululizo wa matokeo mabaya katika Ligi Kuu Bara.

Dar es Salaam. Azam FC imemtangaza kocha wake wa zamani Aristica Cioaba kuwa kocha mkuu mpya akichukua nafasi ya Etienne Ndayiragije anayetarajia kutangazwa kuwa kocha wa kudumu wa timu ya taifa ya Tanzania ‘Taifa Stars’.

Azam imemtangaza Cioaba kupitia akaunti yake ya twitter mchana huu #WelcomeBackCioaba Azam FC tunayofuraha kubwa kuwafahamisha kuwa tumeingia mkataba wa mwaka mmoja na Kocha wetu wa zamani Aristica Cioaba.

“Cioaba anachukua mikoba ya Kocha, Etienne Ndayiragije, ambaye anatarajia kutangazwa kama Kocha wa kudumu wa timu ya Taifa 'Taifa Stars'.”

Cioaba aliondoka Azam 2018, baada ya kushindwa kukubaliana na viongozi wa klabu hiyo kutokana na mfululizo wa matokeo mabaya katika Ligi Kuu Bara.

Baada ya kutimuliwa Cioaba nafasi yake ilichukuliwa na aliyekuwa kocha wa Singida United, Hans van Pluijm.

Kutangazwa kwa Cioaba leo kunamaliza uvumi wa muda mrefu wa hatma ya kocha Ndayiragije ambaye tangu amejiunga na Azam alikuwa na jukumu la kuwa kaimu kocha mkuu wa Taifa Stars.