Biashara Utd yanusa Ligi Kuu

Muktasari:

  • Kocha huyo amewahakikisha mashabiki mkoa Mara kuwa msimu ujao timu hiyo itapanda Ligi Kuu

 Kocha wa Biashara United, Omary Madenge  amewaambia mashabiki wake watazidi kufurahi kwani mambo mazuri yanakuja ndani ya timu hiyo.

Biashara United iliwatandika Alliance FC kwa mabao 2-0 katika mchezo wa Ligi Daraja la Kwanza (FDL)mtanange uliopigwa kwenye Uwanja wa Kumbukumbu ya Sokoine, Mara.

Biashara United inaongoza Kundi C ikiwa na pointi 23, wakiwafuatiwa na Dodoma FC (21), huku Alliance ikiwa ya tatu na pointi 19.

Kocha Madenge alisema msimu ujao mashabiki wa soka wa mkoa wa Mara wategemee klabu hiyo kupanda Ligi Kuu kwani amejipanga kushinda mechi tatu zilizobakia.

Alisema mipango yao ni kuhakikisha wanarudisha heshima ya mkoa huo kwa kuipandisha Biashara United Ligi Kuu msimu ujao.

“Mashabiki waendelee kutupa sapoti tumejipanga msimu huu kupandisha timu Ligi Kuu tumebakiza mechi tatu ambazo zote lazima tushinde”alisema Madenge.

Mara ya mwisho Mkoa wa Mara kuona Ligi ilikuwa ilikuwa mwaka 2003 ambapo timu ya Polisi Mara ilikuwa ikishiriki mashindano hayo.