Kotei kutambulishwa rasmi Kaizer Chiefs

Muktasari:

Kiungo huyo alishinda tuzo ya kiungo bora wa mwaka wa Simba katika sherehe za Simba MO award.

Dar es Salaam. Kiungo bora wa Simba msimu uliopita Mghana James Kotei anatarajia kutambulishwa katika klabu yake mpya ya Kaizer Chiefs inayoshiriki Ligi Kuu Afrika Kusini, baada ya kukubaliana kusaini mkataba wa miaka miwili.

Kiungo huyo alikuwa na wakati mzuri na kikosi cha Simba, ameachana na klabu hii baada ya mkataba wake kumalizika huku jina lake likiondolewa kwa wachezaji wanaohitajika kwaajili ya msimu ujao.

Hali hiyo iliwashangaza wapenzi na mashabiki wa Simba baada ya kusikia mchezaji huyo anatemwa licha ya kwamba alichaguliwa kuwa kiungo bora wa msimu katika tuzo za Mo Awards.

Hata hivyo mabosi wa Kaizer walitambua huduma ya mchezaji huyo na juzi Jumatatu walifanikiwa kusaini mkataba wa miaka miwili kwaajili ya kupata huduma ya Mghana huyo.

Mwanaspoti lilimtafuta Kotei na kutaka kufahamu ukweli uliopo, alisema “Kila kitu kimeenda poa na leo itakuwa rasmi na kila mtu atafahamu,” alisema Kotei.