Fainali ya Nadal, Djokovic yanukia

Muktasari:

  • Nadal bingwa mtetezi wa US Open ambaye mwaka jana alimshinda Kevin Anderson katika fainali jana alitinga nusu fainali kwa kishindo na sasa amebakiza kigingi kimoja cha leo jioni ili kutinga fainali kwa mara ya pili mfululizo

New York, Marekani. Kuna uwezekano mkubwa fainali ya mwaka huu ya US Open kwa wanaume ikawakutanisha Rafael Nadal na Novak Djokovic.

Nadal bingwa mtetezi wa US Open ambaye mwaka jana alimshinda Kevin Anderson katika fainali jana alitinga nusu fainali kwa kishindo na sasa amebakiza kigingi kimoja cha leo jioni ili kutinga fainali kwa mara ya pili mfululizo

Iwapo wawili hao watashinda mechi zao na nusu fainali watakutana kwenye fainali ikiwa ni  mara yao ya 53 kukutana na ikitokea hivyo fainali ya mwaka huu itakuwa yenye mvuto wa aina yake kutokana na uwezo wa wote wawili.

Nadal anayeshika nafasi ya kwanza kwa ubora kwa wanaume na Djokovic anayerejea kwenye kiwango chake anashika nafasi ya 12, licha ya kurejea dimbani miezi mitatu iliyopita akitokea kuuguza bega lililomuweka nje ya dimba kwa karibu mwaka.

Katika nusu fainali leo Nadal atamkabili kwa mara ya pili kwa mwaka huu kwenye mashindano makubwa ya Grand Slam, shujaa wa tenisi kutoka Argentina, Juan Martin del Potro wakati Djokovic atachuana na Kei Nishikori kutoka Japan katika nusu fainali ya pili.

Licha ya ugumu wa Del Potro aliyetumia saa 4:49 kwenye uwanja wa Flushing Meadows, kumng’oa Dominic Thiem katika robo fainali lakini hatarajiwi kumshinda Nadal, mshindi mara tatu wa US Open.