Fifa yamuongezea kibano Kwesi Nyantakyi

Muktasari:

  • Nyantakyi alilazimika kujiuzulu wadhifa wote wa kisoka kuanzia uongozi wa GFA pamoja na ule wa Caf na Fifa, kutokana na kuibuliwa kwa madai ya kashfa ya rushwa na ufisadi dhidi yake.

Zurich, Uswisi. Bosi wa zamani wa Chama cha soka cha Ghana, Kwesi Nyantakyi, amezidi kuminywa na Shirikisho la soka la kimataifa (Fifa).

Nyantakyi alilazimika kujiuzulu wadhifa wote wa kisoka kuanzia uongozi wa GFA pamoja na ule wa Caf na Fifa, kutokana na kuibuliwa kwa madai ya kashfa ya rushwa na ufisadi dhidi yake.

Kiongozi huyo alihukumiwa kujiweka kando na masuala ya soka kwa siku 90 Juni 8 mwaka huu, ameongezewa siku nyingine 45 zaidi za adhabu.

Kamati ya maadili ya Fifa ilimkuta Nyantakyi na kosa la kupokea fedha zinazoaminika kuwa za rushwa ingawa yeye alijitetea kuwa hiyo ilikuwa zawadi kutoka kwa jamaa yake.

Alidaiwa kujichanganya kuhusu kiasi cha Dola 65,000 za Marekani alizobambwa nazo mwandishi wa habari, Anas Aremeyaw Anas, fedha ambazo alishindwa kuzitolea maelezo ya kina.