Fulham yampa ulaji Solskjaer

Muktasari:

  • Ushindi wa mabao 3-0 iliyopata Manchester United dhidi ya Fulham imemsafishia njia kocha wa muda Ole Gunnar Solskjaer.

London, England. Fulham inaweza kuwa ndio imempa ulaji Ole Gunnar Solskjaer Manchester United.

Matokeo mazuri iliyopata Man United dhidi ya Fulham Jumamosi iliyopita, yawavutia mabosi wa klabu hiyo ya Old Trafford.

Man United ikiwa katika ubora wake, ilipata ushindi huo na kukwea hadi nafasi ya nne katika msimamo wa Ligi Kuu England.

Solskjaer amewavutia wamiliki wa Man United, baada ya kushinda mechi 10 kati ya 11 tangu alipotwaa mikoba ya Jose Mourinho.

Solskjaer anatarajiwa kupewa mkataba wa kudumu muda mfupi ujao kutokana na kazi nzuri.

Mwenyekiti Avram Glazer alizungumza na Solskjaer muda mfupi baada ya Man United kuifunga Fulham.

Avram anatarajiwa kuzungumza na mwenyekiti mwenza Joel Glazer kuhusu mkataba wa nyota huyo wa zamani wa Man United.

Awali, Kocha wa Tottenham Hotspurs Muargentina Mauricio Pochettino alikuwa akipewa nafasi ya kutwaa nafasi hiyo.