Ghafla! Fei Toto amsahau Gadiel Michael

Muktasari:

Kiungo wa Yanga, Fei Toto amesema, kuondoka kwa beki wa pembeni Gadiel Michael aliyehamia Simba kwao si kitu na wameshamsahau.

SIKU chache baada ya beki wa kushoto, Gadiel Michael kutimkia Simba, kiungo wa Yanga Feisal Salum 'Fei Toto' amesema tayari wameshamsahau na sasa wanaangalia ni namna gani kikosi chao kitafanya vizuri msimu ujao.
Gadiel amejiunga na Wekundu hao wa Msimbazi baada ya kumaliza mkataba wake Yanga ambao ulikuwa wa miaka miwili.
Akizungumza na Mwanaspoti, Fei Toto alisema kila mchezaji ana umuhimu wake anapokuwa kikosini akiondoka tu ni rahisi kusahaulika hasa akipatikana mbadala wa mchezaji huyo.
"Gadiel alikuwa mchezaji mwenzetu, amemaliza kandarasi yake na hakupenda kuongeza mkataba ameamua kuondoka, kwa hiyo kuna maisha mengine baada ya hili. Sisi tumeshamsahau ni kama historia kwetu", alisema Fei Toto.
"Unajua maisha ya soka ni popote unaweza ukawa muhimu sana kikosini na ukawa na msaada mkubwa lakini ukiondoka watu wanasahau,  wanaangalia mambo mengine ndivyo ilivyo kwa upande wetu unapomzungumzia Gadiel," alisema Fei Toto.