Hilo dau la Real Madrid kuinasa saini ya Kylian Mbappe ni kufuru

REAL Madrid inajiandaa kufanya kufuru kwa kutoa dau la Pauni 257 milioni ili kunasa saini ya straika wa Paris Saint-Germain, Kylian Mbappe, 21, wakati wa dirisha kubwa la usajili Juni mwaka huu.

Inaelezwa baada ya kukaa PSG kwa miaka mitatu, Mbappe sasa yuko tayari kujiunga na Real Madrid ili kupata changamoto mpya katika ligi yenye ushindani mkubwa zaidi ya Ufaransa.

Licha ya Mbappe kubakiza miaka miwili na nusu kwenye mkataba wake wa sasa PSG, Real Madrid inajiandaa kuvunja rekodi ya usajili ili kunasa saini ya straika huyo.

Madrid imepanga kuweka mezani Pauni 257 milioni ili kumnasa Mbappe, dau ambalo litavunja rekodi ya sasa ya usajili ya Pauni 198 milioni ambayo PSG ilitumia kumsajili Neymar kutoka Barcelona.

Mbappe amekuwa na wakati mzuri kwenye kikosi cha PSG na klabu nyingi kubwa barani Ulaya zimekuwa zikihusishwa na kuitaka huduma zake ikiwamo Liverpool. Hata hivyo, kinachosubiriwa ni kwa klabu yenge nguvu na Madrid inaonekana itaishinda vita hiyo.