Juuko,Wawa waanza na Waarabu, Kagere mmh!

Muktasari:

  • Huo ni mchezo wa kwanza wa hatua ya makundi ya Ligi ya Mabingwa Afrika kwa Simba.  Simba imepangwa Kundi D, pamoja na timu za Vita Club ya Congo, Al Ahly ya Misri na JS Saoura ya Algeria.

Dar es Salaam.  Kocha Mkuu wa Simba,  Mbelgiji Patrick Aussems amewaanzisha Juuko Murshid na Pascal Wawa kucheza beki ya kati huku Meddie Kagere akitupwa benchi.

Aussems amemchezesha Juuko na Wawa kwa mara ya kwanza katika mchezo wa leo Jumamosi wa Ligi ya Mabingwa Afrika dhidi ya JS Saoula ya Algeria kwenye Uwanja wa Taifa jijini Dar es Salaam.

Hii ni baada ya Erasto Nyoni kuumia katika mshindano ya Kombe la Mapinduzi kwani Juuko raia  wa Uganda hakuwa na nafasi ya kucheza.

Awali, Nyoni ndiye alikuwa akicheza na Wawa raia wa Ivory Coast.

Kwa upande wa Kagere alikuwa akipangwa kuanza kikosi cha kwanza katika sehemu kubwa ya mechi zake lakini sasa ataanzia benchi na kusubiri litakalotokea mchezoni.

Wachezaji wengine kipa ni Aishi Manula, beki us kulia anacheza Nicolas Gyan na kushoto ni Mohammed Hussein 'Tshabalala' kati ni hao,  Wawa na Juuko.

Viungo ni Hassan Dilunga, Jonas Mkude na Mghana James Kotei. Washambuliaji ni Emmanuel Okwi raia wa Uganda, John Bocco 'Adebayor'na Mzambia  Cletous Chama.