Kimbunga Ronaldo chaikumba Lithuania

Muktasari:

Ronaldo mwenye hat trick nane na mabao 93 aliyofunga kwa ujumla akiwa na Ureno anashikilia rekodi ya kuwa mfungaji bora wa michezo ya kuwania nafasi ya kushiriki Fainali za mataifa ya Ulaya maarufu kama EURO.

Kocha wa timu ya Taifa ya Ureno, Fernando Santos anaamini mabao manne yaliyofungwa na Cristiano Ronaldo kwenye mchezo dhidi ya Lithuania yametosha ‘bila shaka’ kuwa ndiye mchezaji bora zaidi duniani kwa sasa.

Ronaldo amekuwa  mfungaji bora wa muda wote wa Ureno katika michezo ya kuwania nafasi ya kufuzu kwa fainali za Mataifa ya Ulaya, akiwa na mabao 25 baada ya kuiongoza  Ureno kuibuka na ushindi wa mabao  5-1 mbele ya Lithuania.

Nyota huyo mwenye umri wa miaka 34,  alionyesha ubora wake  katika mchezo huo wa kundi B wa kuwania nafasi ya kucheza fainali za mataifa ya Ulaya kwa mwaka 2020  kwenye mji wa Vilnius ambapo alifikisha hat-trick yake ya nane akiwa na timu yake ya Taifa.

"Bila shaka imetosha kuonyesha ni mchezaji bora zaidi Duniani. Hakuna uwanja ambao tutaenda asikubalike, tulienda Paris, ulikuwa mchezo wangu wa kwanza nchini Ufaransa katika Hotel ambayo tulifikia, ilizungukwa na watu kibao madirishani,” alisema kocha huyo.

Santos aliendelea: "Huwa najisikia vibaya asipofunga. Atasema unadhani huu ni mwisho… Hakuna mwisho. Uwe tayari muda wowote kwa sababu hakuna mwisho.”

Maajabu ya Ronaldo yalianza ndani ya dakika saba pale Ureno ilipopata penati, nyota huyo wa Juventus alipiga vyema pigo lile kwenye kona ya kulia na kuitanguliza timu yake ya Taifa kabla ya kufunga mengine kipindi cha pili.

Mabeki wa Lithuania walikiona cha moto kipindi hicho cha pili ambapo walishindwa kumzuia mchezaji huyo wa zamani wa Manchester United na Real Madrid kwa kupachika mabao mengine kwenye dakika ya 61, 65 na 76.

Ronaldo anashikilia tuzo tano za mchezaji bora wa Dunia, Ballon d'Or sawa na Lionel Messi ambaye ni nahodha wa FC Barcelona. Kwa sasa tuzo hiyo kubwa na heshima inayotoka kila mwaka, inashikiliwa na Luka Modrić wa Real Madrid.