Kocha Al Ahly adai joto, kujiangusha nyota Simba sababu ya kipigo chao

Muktasari:

  • Simba imeweka rekodi ya kushinda mechi zake zote za Ligi ya Mabingwa kwenye Uwanja wa Taifa

Cairo, Misri. Kocha wa Al Ahly, Martin Lasart amesema sababu ya timu yake kucheza kiwango duni na kufunga bao 1-0 na Simba jana kimetokana na hali ya hewa ya joto kali, lakini anaamini timu yake itafuzu kwa robo fainali.

Ahly ilipata pigo baada ya kufungwa bao katika kipindi cha pili na mshambuliaji Meddie Kagere wa Simba ikiwa ni kipigo cha kwanza kwa mabingwa hao wa kihistoria wa Ligi ya Mabingwa katika hatua ya makundi.

Pamoja na kipigo hicho, Al Ahly imeendelea kuongoza Kundi D ikiwa na pointi saba, moja zaidi kwa Simba inayoshika nafasi ya pili ikifuatiwa na JS Saoura (5) na AS Vita ikiwa ya mwisho na pointi 4.

"Tumecheza katika joto kali na mazingira ambayo siyo rafiki," alisema Lasarte baada ya mechi hiyo.

"Hali ya hewa mbaya hasa katika kipindi cha pili iliwaathiri wachezaji wetu na kuchoka zaidi."

"Niliwachezesha viungo watatu wakabaji ili kuepuka madhara."

Kocha huyo Uruguayan pia aliwashutumu wachezaji wa Simba kwa kucheza mbinu yao kupoteza muda "haukuwa mchezo wa kiungwana kabisa."

"Wachezaji wa Simba walijiangusha zaidi ya mara 15 uwanjani kwa lengo la kupoteza muda," aliongeza.

Kocha huyo mwenye miaka 57, anaamini mabingwa hao mara nane watafuzu kwa robo fainali na hatimaye kutwaa ubingwa wa kwanza wa mashidano hayo tangu ilipofanya hivyo 2013.

"Ahly wakati wote tunaangalia mbele. Lengo letu ni kushinda mechi zetu mbili zinazokuja ili kutimiza ndoto yetu ya kutwaa ubingwa huu."

Ahly watakuwa ugenini DR Congo kuwavaa Vita Club hapo Machi 8, kabla ya kuwapokea JS Saoura ya Algeria siku nane baadaye katika mchezo wa mwisho.