Kwa beki huyu wa Yanga! Kagere, Bocco wajipange

KULE Msimbazi kwa sasa kumekuwa na kejeli. Mashabiki wa klabu ya Simba wanaubeza usajili unaofanywa na watani zao wa Yanga, wakidai eti ni kama wa makusanya tu. Hii ni kwa sababu kila uchao zinaripotiwa taarifa za nyota flani kutoka nje ya nchi amemwaga wino ama majembe ya ndani nayo yamenaswa na mabosi wapya wa Yanga.

Hata hivyo, kama Simba wanajidanganya kwamba Yanga inasomba tu wachezaji wapya bila mipango, basi itakula kwao, kwani mabosi hao wa Jangwani hawajakurupuka kusainisha majembe hayo na wengine wanaoendelea kushushwa na klabu hiyo.

Achana na nyota waliosainishwa kutoka ndani ya Tanzania, Yanga imeshusha vifaa vya maana kutoka nje ya nchi wakiwamo mastraika wawili wakali, Maybin Kalengo kutoka Zambia na Mnamibia Sadney Urikhob.

Pia, imewasaini mawinga kutoka Rwanda, Patrick Sibomana na Issa Bigirimana, pia kuna beki mmoja wa kati matata Lamine Moro na mwingine fundi zaidi Seleman Moustafa kutoka Burundi.

Sasa unaambiwa achana na Lamine. Wapotezee Urikhob, Kalengo ama kina Bigirimana, Msimbazi na timu nyingine pinzani lazima zijipange hasa safu yao ya ushambiliaji mbele ya Moustafa aliyetokea Aigle Noir FC inayotokea mji wa Makamba.

Beki huyo wa kati (19) ametajwa ni mmoja kati ya mabeki wenye roho mbaya katika kuwazuia washambuliaji wasumbufu, hivyo kina Meddie Kagere, John Bocco lazima wajipange siku ya mechi ya watani.

Rekodi zinaonyesha tangu mwaka 2016, Yanga haijaonja ushindi mbele ya Simba kwani ushindi wa mwisho ulikuwa katika mechi ya Februari 20, pale Donald Ngoma na Amissi Tambwe walipowanyamazisha Msimbazi kwa mabao 2-0.

Baada ya hapo Simba imewaburuza Yanga kwa kushinda mechi tatu na tatu nyingine kumalizika kwa sare, huku straika wa mwisho kuwaliza akiwa ni Kagere aliyetupia kambani bao pekee wakati Msimbazi wakiwalaza mapema Jangwani Feb 16.

SASA WAJIPANGE

Hata hivyo, inaelezwa usajili wa Moustafa na Lamine watakaoungana na kina Kelvin Yondani na Andrew Vincent ‘Dante’ na Abdallah Shaibu ‘Ninja’ unaweza kuwa mwisho wa unyonge kwa Yanga kama sifa alizopewa beki huyo Mrundi ndivyo vilivyo.

Kwa sifa hizi za beki mpya wa Yanga, Suleyman Mustafa kutoka Burundi, basi kina Meddie Kagere, Emmanuel Okwi na John Bocco wa Simba, wanatakiwa kujipanga vilivyo msimu ujao, unaambiwa anakaba haachi hata mpenyo kwa wapinzani.

Baadhi ya nyota wanaotokea Burundi, wamezungumza na Mwanaspoti na kuanika wasifu wa beki huyo wa kati kuwa ni mtu wa kazi na Yanga wamelamba dume kwa kumnyakua kwani washambuliaji wa timu pinzani kwa sasa watakuwa na kazi ya ziada kuitungua.

Straika wa Yanga, Amissi Tambwe alisema japo bado hana hakika kama Yanga imemsajili Moustafa kwa vile anasikia tu hewani, lakini Mrundi mwenzake huyo ni bonge la beki licha ya umri mdogo alionao. Mustapha ana miaka 19 tu kwa sasa, kwani Septemba 6, ndio atatimiza miaka 20 kamili panapo majaliwa.

Tambwe alisema kazi aliyoifanya beki huyo ndani ya Timu ya Taifa ya Vijana U20 na hata ile ya wakubwa ya Intamba Murugamba ni wazi itawatoa jasho washambuliaji wa timu pinzani msimu ujao.

Alisema anatambua uwezo wa Mustapha kwenye klabu kadhaa alizochezea kwao na hata timu ya taifa na kuthibitisha alivyo noma, aliisaidia klabu yake kuandika historia na kubeba taji la Ligi Kuu ya Burundi na kukata tiketi ya kimataifa msimu ujao. Katika mechi 30 za Ligi Kuu ya Burundi maarufu kama Ligue A, Aigle imemaliza msimu kwa kufunga mabao 72 na kuruhusu 26 ikiwa ndio timu iliyofungwa mabao machache.

“Anacheza Timu ya Taifa ya Burundi na sio wa kukaa benchi, kama watakuwa wamemsajili basi hawajakosea atawasaidia kwenye Ligi Kuu Bara na michuano ya kimataifa,” alisema Tambwe aliyefunga zaidi ya mabao 60 katika misimu sita ya Tanzania Bara.

Naye Bigirimana Blaise aliyetua Namungo FC iliyopanda Ligi Kuu msimu ujao akitokea Alliance, alisema Moustafa ana uwezo wa kumiliki mpira, anatumia nguvu na akili pamoja na kupandisha mashambulizi.

“Namjua Moustafa tangu akiwa mdogo ni mchezaji mzuri, ndio maana anaichezea timu ya taifa, kutua kwake Yanga ataisaidia hasa kwenye michuano ya kimataifa ambayo watacheza kwa mwaka huu.

“Ingawa kila kocha ana mifumo yake na chaguo lake, ila ninavyomfahamu Moustafa ni mchezaji mwenye uwezo wa juu sijamuona beki wa kumweka benchi ndani ya Yanga,” alisema straika huyo aliyewahi kutamba na Stand United.

Blaise alisema uwezo wake ni wakukabana na washambuliaji wasumbufu na wenye uchu wa kuzifumania nyavu kama Kagere, John Bocco na Emmanuel Okwi wa Simba: “Kwa kifupi washambuliaji wasumbufu watawezana na beki huyo ana nguvu, hakuachii nafasi na ana uwezo wa kupandisha mashambulizi.”

MAYAY NAYE

ACHAMBUA

Mchambuzi wa soka, Ally Mayay alitoa alisema usajili unaoendelea Yanga kama unafanywa chini ya Kocha Zahera anaamini utakuwa na manufaa na kuisaidia klabu hiyo.

Aliishauri Kamati ya Usajili ya Yanga, kuepuka kusajili wachezaji wanaowataka wao badala yake aliwataka wawe watekelezaji wa ripoti ya Kocha Zahera anachokitaka kwa msimu ujao na michuano ya kimataifa.

“Kama kamati itakuwa inasajili wachezaji wake, basi wanampa Zahera cha kujitetea, lakini kama atasajili yeye ndiye atakayebeba mzigo wa lawama endapo akishindwa kufikia malengo ya klabu.

“Msimu uliopita Zahera aliweka wazi amesajiliwa wachezaji asiowahitaji, unaona kiasi gani ambavyo alionekana hana hatia ya kulaumiwa, kubwa zaidi Yanga isajili wachezaji wa kimataifa na sio ligi ya ndani, wamepata nafasi hiyo wanapaswa kwenda kufanya kweli.

“Mfano Abdull Aziz Makame uwezo wake unajulikana, pia Wanyarwanda ni wazuri niliwaona kwenye mashindano ya CECAFA, lakini hao wengine ambao wanawatazama kupitia mitandao sina lolote la kusema hapo.”