Lunyamila: Amtabiria Molinga makubwa Yanga

Dar es Salaam. Nyota wa zamani wa Yanga, Edbily Lunyamila amesema mshambuliaji David Molinga akiendelea na kasi ya kuzifumania nyavu katika mechi za ligi anaamini atabadili upepo.

Lunyamila alisema anaamini Molinga ni mfungaji mzuri anachomshauri ni kuongeza juhudi ya kufanya mazoezi ya kumfanya mwili wake kuwa mwepesi akiamini atafunga mabao mengi.

 "Nimemfuatilia katika mechi za kirafiki anazocheza namuona anajua kucheza na nyavu, naamini atabadili upepo katika ligi tofauti na alivyopokelewa na mashabiki wakati anafika."

"Kocha Mwinyi Zahera akimbadilisha kidogo baadhi ya Molinga, atafunga na watu watashangaa, pia yeye mwenyewe aongeze bidii ya mazoezi atafika mbali badala ya kumchukulia poa atabadili upepo na kuwa mfalme,"alisema.

Molinga amefunga mabao mawili ya Ligi Kuu Bara, aliyofunga dhidi ya Polisi Tanzania, Yanga ikitoka sare ya mabao 3-3, manne amefunga kwenye mechi za kirafiki, hivyo ana jumla ya mabao sita.