Lwandamina: Yanga itatupa upinzani

Muktasari:

Lwandamina aliiongoza Yanga kutwaa ubingwa wa Ligi Kuu Tanzania Bara msimu wa 2016/2017 kabla ya kurejea Zambia kuinoa Zesco

KOCHA wa Zesco United, George Lwandamina ametabiri mechi yao dhidi ya Yanga kesho Jumamosi kuwa ngumu kutokana na mabadiliko ambayo wapinzani wao wamepitia.
Lwandamina ambaye aliwahi kuinoa Yanga hapo awali, alisema anaamini wawakilishi hao wa Tanzania wamekuwa na mabadiliko makubwa katika kipindi ambacho kimepita tangu walipoachana.
"Naamini kuna mabadiliko ambayo Yanga wamepitia, kuna wachezaji wapya lakini pia hata sisi Zesco kuna mabadiliko tumepitia kwenye timu yetu.
"Kutokana na hilo naamini mechi itakuwa nzuri na tumejipanga vyema kukabiliana na Yanga tukifahamu kwamba mechi itakuwa ngumu," alisema Lwandamina.
Lwandamina hadi anaondoka Yanga, alikuwa ameiongoza kutwaa ubingwa wa Ligi Kuu msimu wa 2016/2017.
Kocha huyo aliondoka kutokana na changamoto ya kiuchumi na kuamua kurejea Zesco United anakofundisha hadi sasa.