Majimaji kujaribu moto wa Mabingwa watetezi Mapinduzi

Muktasari:

Nyota wanne waliokosekana kikosini Majimaji wamerudi na kumpa matumaini kocha wao kuibuka na ushindi.

Mbeya. Kocha Mkuu wa Majimaji FC, Peter Mhina amesema kikosi chake kipo vizuri kuelekea mchezo wao dhidi ya Mabingwa watetezi wa Mapinduzi, Azam FC utakaochezwa leo Alhamisi kwenye Uwanja wa Majimaji Songea.

Kocha Mhina alisema wanaiheshimu Azam kutokana na kuwa katika nafasi nzuri katika msimamo lakini dakika 90 ndiyo mwamuzi wa mwisho kwa mechi hiyo.

Alisema, “Tunaendelea na mazoezi kwa ajili ya mechi zetu mbili zilizo mbele yetu lakini haswa ni hii inayochezwa Alhamisi, tumejipanga kwa ajili ya kuchukua pointi tatu dhidi ya mabingwa hawa wa Mapinduzi.”

Mhina alisema kufungwa mechi mbili mfululizo kumewapa somo la kurekebisha makosa yaliyoonekana na kuhakikisha wanapata pointi tatu muhimu kwa kila mechi.

“Ingawa nimeichukua timu hii baadaye lakini kadri siku zinavyozidi kwenda wachezaji wanazidi kuzoea mifumo yangu na mbinu zangu, kwa hiyo ni imani yangu kwamba hawataniangusha siku hiyo.”

Aliongeza “Ongala aliiongoza timu hii kwa misimu miwili kwa hiyo kuwabadilisha wachezaji siyo kazi ndogo na ndiyo maana nimewapima kwa kucheza mechi kadhaa za kirafiki kwenye kipindi hiki cha mapunziko,” alisema Mhina.