Makambo atoswa DR Congo

Muktasari:

  • Jina la Makambo lilitajwa katika orodha ya awali ya wachezaji 40 lakini katika orodha ya mwisho kuelekea mchezo dhidi ya Liberia, mshambuliaji huyo wa Yanga amekosekana

Dar es Salaam. Wakati timu ya Taifa ya Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo (DRC) ikitangaza kikosi cha nyota 25 kwa ajili ya mechi ya kuwania kufuzu fainali za Afrika (AFCON) dhidi ya Liberia, Machi 24 jijini Kinshasa.

Makambo inasemekana alikuwemo kwenye kikosi cha awali cha nyota 40 ambao sasa wamechujwa na kocha Florent Ibenge na kubakia 25 ambao miongoni mwao ndio watapeperusha bendera ya nchi hiyo katika mchezo huo muhimu.

Kama ilivyo kwa Makambo, hakukuwa na nafasi pia kwa mshambuliaji wa Fulham inayoshiriki Ligi Kuu ya England, Neeskens Kebano kama ilivyo kwa nyota wa Middlesbrough, Assombalonga Britt.

Kocha Ibenge pia amemfungia vioo nyota wa Astana ya Kazakhstan, Junior Kabananga kama alivyofabya kwa mshambuliaji Jean-Makusu Marc Mundele anayechezea klabu anayoifundisha ya AS Vita.

Uteuzi wa kushtukiza kwenye kikosi cha DRC ni ule wa mshambuliaji mkongwe mwenye umri wa miaka 33,Tresor Mputu wa TP Mazembe ambaye amekuwa akifanya vyema kwenye hatua ya makundi ya Ligi Ya Mabingwa Afrika msimu huu.

Kwenye hatua ya makundi ya Ligi ya Mabingwa Afrika msimu huu, Mputu ndiye mchezaji anayeongoza kwa kupiga idadi kubwa ya pasi za mabao ambapo amepiga pasi nne huku pia akifunga mabao matatu.

Kikosi kamili cha DRC kinaundwa na makipa Auguy Katembwe, Anthony Mossi na Ley Matampi wakati mabeki ni Christian Luyindama, Arthur Masuaku, Marcel Tisserand, Beaudrick Ungenda, Glody Ngonda, Padou Bompunga, Issama Mpeko na Djuma Shabani.

Viungo ni Youssouf Mulumbu, Chancel Mbemba, Jacques Maghoma, Marveille Bope, Ngoma Fabrice, Nelson Munganga na Paul Mpoku huku Washambuliaji wakiwa ni Tresor Mputu, Yannick Bolasie, Bakambu Cedric, Diumerci Mbokani na Jonathan Bolingi