Manchester City yapata pigo kabla ya kuivaa Liverpool

Muktasari:

Ederson amezua hofu kuwa huenda asiwe sehemu ya kikosi cha Pep Guardiola ambao wanasafari ya kwenda Anfield kucheza mchezo huo, Jumapili wa Ligi Kuu England.

London, England. Manchester City wameingiwa na hofu kutokana na majeraha aliyoyapata kipa wao namba moja, Ederson dhidi ya Atalanta katika mchezo Ligi ya Mabingwa Ulaya ikiwa zimesalia siku chache kabla ya kukutana na Liverpool.

Kipa Ederson alipata majeraha ya misuli na kufanyiwa mabadiliko mapumziko wakati Manchester City na Atalanta wakiwa sare ya bao 1-1 na nafasi yake akaingia Claudio Bravo, alionyeshwa kadi nyekundu.

Ederson amezua hofu kuwa huenda asiwe sehemu ya kikosi cha Pep Guardiola ambao wanasafari ya kwenda Anfield kucheza mchezo huo, Jumapili wa Ligi Kuu England.

"Tunaimani na Claudio, namjua vizuri kwanini niwe na  hofu na wachezaji wangu, kuna mambo kadhaa tu ambayo tunatakiwa kuyaweka sawa. Naamini Claudio yupo tayari kwa mchezo," alisema

Guardiola aliendelea kwa kutoa ufafanuzi kuwa, "Ederson alisumbuliwa na misuli, tukaona apumzike kwa sababu alianza kujisikia hovyo mwishoni mwa kipindi cha kwanza, hajapata majeraha makubwa."

Aliyekuwa kivutio katika mchezo uliomalizika kwa sare ya bao 1-1 dhidi ya Atalanta  kwa upande wa Manchester City, alikuwa Kyle Walker ambaye ilibidi akadake baada ya Bravo kuonyeshwa kadi nyekundu.

Licha ya kuzoelekea kucheza kama beki wa kulia, akiwa golini, Walker aliokoa michomo miwili.