Manchester United yamvuruga Lampard

Muktasari:

  • Kocha wa Chelsea, Frank Lampard, ameanza vibaya kibarua chake baada ya timu yake kubugizwa mabao 4-0 dhidi ya Manchester United.

London, England. Frank Lampard ameanza vibaya kazi yake mpya katika Ligi Kuu England, baada ya Chelsea kupata kipigo cha aibu kwa kufungwa mabao 4-0 dhidi ya Manchester United, jana.

Lampard amesema makosa manne ya wachezaji wake yamechangia kipigo cha mabao manne waliyonyukwa juzi usiku dhidi ya Manchester United katika mchezo wa Ligi Kuu England.

Man United ikiwa nyumbani Old Trafford ilianza vyema msimu mpya baada ya kuigagadua Chelsea mabao 4-0, ikiwa ni mechi ya kwanza kwa Lampard.

“Makosa manne yalitugharimu, wenzetu walishambulia kwa mipira mrefu ya kushitukiza, kipindi cha kwanza tulikuwa mbele yao, adhabu ya kutokusajili na majeruhi ya wachezaji nayo yamechangia lakini sitaki kutoa kisingizio hicho,”alisema Lampard.

Kocha huyo wa zamani wa Derby County alisema aliboresha kikosi kwa kumuingiza N’golo Kante ili kuongeza nguvu katika eneo la kiungo, lakini jahazi lake lilizama.