Mashujaa yataka kuendeleza ubabe kwa Simba

Muktasari:

Mashujaa mapema mwaka huu iliisambaratishja Simba 3-2 kwenye mchezo wa Kombe la FA uliochezwa kwenye Uwanja wa Taifa

Dar es Salaam. Kocha Mkuu wa Mashujaa FC, Atuga Manyundo amesema anataka kuandika rekodi ya aina yake katika mchezo wa kirafiki leo Jumatatu dhidi ya Simba utakaopigwa Uwanja wa Lake Tanganyika, mkoani Kigoma.

Manyundo alisema mchezo huo unatumika kama maandalizi ya kukinoa kikosi chake kuelekea mchezo wa Ligi Daraja la Kwanza (FDL) mwishoni mwa wiki hii atakapokuwa ugenini kucheza na Transit Camp Uwanja wa Isamuhyo.

"Mchezo huo ni fursa kwa vijana wangu kuendelea kujitangaza na kuonekana na timu nyingine kwa sababu soka ni ajira na sitegemei kumuona mchezaji miaka inapita anaendelea kubaki katika kiwango kile kile, lazima akue ili mambo yabadilike," alisema Manyundo.

Mashujaa mapema mwaka huu iliisambaratishja Simba 3-2 kwenye mchezo wa Kombe la FA uliochezwa kwenye Uwanja wa Taifa na kuitupa nje timu hiyo ambayo ni mabingwa mara mbili mfululizo wa Ligi Kuu Bara.

Katika FDL, Mashujaa FC inakamata nafasi ya tano ikiwa na alama saba, wakati Simba katika Ligi Kuu ikiwa kinara kwa kuvuna alama 12 baada ya kucheza michezo minne.