Mbonde aahidi makubwa uwanjani msimu ujao

Muktasari:

  • Mbonde alisajiliwa na Simba akitokea Mtibwa Sugar kwa mkataba wa miaka miwili, amecheza msimu mmoja kwa mafanikio na kuanza kusumbuliwa na majeraha kwa muda mrefu.

Dar es Salaam. Baada ya kukaa nje kwa muda mrefu beki wa Simba, Salim Mbonde amesema bado ananafasi ya kuendelea kucheza Ligi Kuu Bara msimu ujao.

Mbonde alicheza Simba mechi ya mwisho kwa dakika 10 tu dhidi ya Kagera Sugar wakifungwa bao 1-0 mbele ya Rais John Magufuli msimu uliopita.

Baadaye Simba ilimpeleka Mbonde kutibiwa Afrika Kusini, lakini tangu msimu huu uanze hajaonekana katika mazoezi ya pamoja hadi sasa.

Mbonde alisema anatarajia kukutana na ushindani kutokana na kukaa nje ya soka muda mrefu, lakini anaamini uzoefu utambeba na ataweza kuendanana kasi inayoendelea.

"Siyo muda muafaka wa kulizungumza hili la ni timu gani nitacheza msimu ujao ninachoweza kusema msimu ujao nitaonekana uwanjani na nategemea kuwa miongoni mwa wachezaji ambao watakuwa na ushindani kutokana na kufanikiwa kulisoma soka nikiwa nje ya uwanja."

"Msimu ulioisha ulikuwa ni mzuri sana na wa ushindani japo kulikuwa na mapungufu kidogo, lakini nawapongeza wachezaji pamoja na viongozi wa klabu zote kwa kupambana na wale waliopoteza nafasi ya kuendelea kucheza ligi kuu wanatakiwa kutambua walikosea wapi wajipange upya kupambana kurudisha timu zao," alisema Mbonde.