Mbunge Chadema ‘ataja sababu’ kipigo cha Taifa Stars

Mbunge wa Mbozi, Pascal Haonga akiomba muongozo kwa Naibu Spika wa Bunge, Dk Tulia Ackson bungeni jijini Dodoma leo, kuhusu kufungwa kwa timu ya Taifa ya Tanzania 'Taifa Stars' na Senegal katika mchezo wao wa kwanza katika Fainali za Mataifa ya Afrika (CHAN).  Picha na Edwin Mjwahuzi

Muktasari:

  • Baada ya Taifa Stars kufungwa mabao 2-0 na Senegal katika Fainali za Mataifa ya Afrika (CHAN) zinazoendelea nchini Misri, mbunge wa Mbozi (Chadema), Pascal Haonga ameibuka bungeni na kuomba mwongozo akihoji sababu za Serikali kuwalipa wachezaji Dola 70 za Marekani badala ya Dola 300.

Dodoma. Mbunge wa Mbozi (Chadema), Pascal Haonga amesema huenda wachezaji wa timu ya Taifa ya Tanzania ‘Taifa Stars’ kulipwa posho kiduchu kumechangia kufungwa mabao 2-0 na Senegal katika mchezo wao kwanza katika Fainali za Mataifa ya Afrika (CHAN) zinazoendelea nchini Misri.

Haonga ametoa kauli hiyo leo Jumatatu Juni 24, 2019 bungeni jijini Dodoma baada ya kuomba mwongozo, akibainisha kuwa kuna tetesi badala ya Serikali kuwalipa wachezaji hao Dola 300 za Marekani, wamelipwa Dola 70.

“Habari zilizopo ni kuwa wamelipwa Dola 70 badala ya Dola 300. Tunaamini unapoingia katika michezo lazima uwe na hali nzuri ya kupambana.”

“Kuna taarifa kwamba kuna siku moja wachezaji hawa hawakufanya mazoezi na kufanya mgomo wa kimya kimya. Kwanini Serikali  haiwapatii posho wachezaji hao kwa sababu michezo  hiyo (CHAN) inaendelea hivi sasa. Tuongoze katika hili kwa nini Serikali isiwapatie fedha,” amesema Haonga.

Akijibu mwongozo huo, Dk Tulia amesema hawezi kujibu kwa kuwa si jambo lililotokea bungeni leo kulingana na kanuni za Bunge zinavyoelekeza.