Messi ndani Barcelona yachapwa, Granada yakalia usukani La Liga

Madrid, Hispania. Kurudi kwa Lionel Messi aliyekuwa majeruhi umeshindwa kuinusuru FC Barcelona kupokea kipigo cha mabao 2-0 kutoka kwa Granada katika  mchezo wa Ligi Kuu Hispania 'La Liga'.

Barcelona wameshindwa kupata matokeo ya ushindi katika michezo yao mitatu iliyopita, waliyocheza ugenini na mwanzo huu, walioanza nao msimu huu, ni mbaya zaidi ambapo Kihistoria mara ya mwisho ilikuwa msimu wa 1994-95.

Katika mchezo huo, Messi aliingia kipindi cha pili, akiwa na kinda Ansu Fati, lakini kuingia kwao hakukuweza kuifanya Barcelona wakomboe bao, ambalo walitanguliwa kipindi cha kwanza kwa kufungwa na Ramon Azeez.

Ndani ya kipindi hicho cha pili, ambacho Messi alikuwepo, FC Barcelona waliruhusu bao lingine dakika ya 66, lililofungwa na Álvaro Cifuentes kwa mkwaju wa penalti.

Nyota wa FC Barcelona, Luis Suarez baada ya kipigo hicho, alisema wanatakiwa kubadilika haraka iwezekanavyo ili kuhakikisha wanarejea kwenye kasi yao ya ushindani.

"Kipigo hiki kimetufanya tuingiwe na hofu ndani yetu,lakini pia  kimetuumiza sana. Tunatakiwa kuimarika kama timu," alisema mshambuliaji huyo wa zamani wa Liverpool.

Kikosi cha Granada kilichocheza  kwenye mchezo huo wakiwa nyumbani ni Silva, V. Diaz, Duarte, Sanchez, Neva, Herrera (Gonalons 83), Montoro, J. Diaz, Azeez, Machis (Vadillo 62) na  Soldado (Fernandez 58)

Upande wa FC Barcelona: Ter Stegen, Semedo, Pique, Lenglet, Firpo (Fati 45), Roberto, de Jong, Rakitic (Vidal 62), Perez (Messi 45), Griezmann na Suarez