Mo Salah anatoka, Mbappe anaingia Anfield

Muktasari:

  • Liverpool wao wanachotamba kwanza watawauzia Real Madrid mchezaji Mo Salah kwa pesa nyingi, kisha watatumia pesa hizo kumbeba Mbappe.

LIVERPOOL imeripotiwa inajiandaa kumpiga bei Mohamed Salah kama itakuwa na uhakika wa kumnasa mshambuliaji wa Paris Saint-Germain, Kylian Mbappe.

Mapema wiki iliyopita kuliibuka taarifa kikosi hicho cha Merseyside kinachonolewa na Jurgen Klopp kipo tayari kuchuana jino kwa jino na Real Madrid katika kuifukuzia saini ya Mbappe kwenye dirisha lijalo la uhamisho wa majira ya kiangazi mwakani.

Wakati Los Blancos wakionekana kuwa na nafasi kubwa kunasa saini ya Mfaransa huyo, Liverpool inajivunia pesa iliyonayo ya kutosha kukamilisha dili hilo.

Liverpool wao wanachotamba kwanza watawauzia Real Madrid mchezaji Mo Salah kwa pesa nyingi, kisha watatumia pesa hizo kumbeba Mbappe.

Mo Salah amekuwa mchezaji muhimu sana huko Anfield, akiwa amefunga mabao manane na kuasisti mara tano katika mechi 14 za michuano yote aliyocheza msimu huu.

Huko nyuma aliwahi kuhusishwa na mpango wa kwenda Real Madrid kitu ambacho kinaweza kutokea kwenye dirisha la majira ya kiangazi mwakani.