Mwadui FC akili yote kwa Yanga

Muktasari:

  • Yanga haina rekodi ya kufungwa na Mwadui kwenye Uwanja wa Uhuru

Kocha msaidizi wa Mwadui FC,Jumanne Ntambi amewatangazia vita Yanga kuwa inyeshe mvua, liiwake jua lazima watachezea kichapo katika mchezo wao Ligi Kuu.

Mwadui iliyopo nafasi ya 10 kwa pointi 12 inatarajia kuwavaa Yanga Januari 17mchezo utakaopigwa kwenye Uwanja wa Uhuru jijini Dar es Salaam.

 Ntambi alisema licha ya mchezo huo kuwa mgumu kutokana na wapinzani wao kuhitaji ushindi, lakini kwa jinsi walivyojiandaa, mabingwa hao wasitarajie mteremko.

Alisema hadi sasa vijana wanaendelea kunolewa vizuri, ikiwamo kuandaliwa kisaikolojia na kusema kuwa wataingia uwanjani kwa mbinu tofauti kuhakikisha wanashinda.

 “Tunajua ni kazi ngumu kutokana na hali ya wapinzani wetu ilivyo, lakini na sisi tumejipanga vilivyo,vijana wanaendelea kupikwa kuhakikisha Yanga wanalala,” alitamba Ntambi.

 

 

Kocha huyo aliongeza kuwa kwa mechi za hivi karibuni, hawajapata matokeo mazuri dhidi ya Yanga, hivyo kazi kubwa itakuwa ni kusaka ushindi ili kuweka heshima na kukaa nafasi nzuri kwenye msimamo.