NYUMA YA PAZIA: Hakuna cha kushangaza kwa Ronaldinho

NIKUSIMULIE kidogo kuhusu mtu aliyeitwa Mane Garrincha. Mtu ambaye Wabrazil wanaamini alikuwa na kipaji kikubwa kuliko Pele. Mtu ambaye kaburi lake mpaka sasa pale Pau Grande Brazil limeandikwa ‘Hapa amelala mmoja kati ya watu ambaye alikuwa furaha ya watu-Mane Garrincha’.

Garrincha alizaliwa mguu wake mmoja ukiwa mfupi kidogo, lakini alikuwa na kipaji cha ajabu cha soka. Pele alitangulizwa mbele baada ya kufanya mambo makubwa akiwa na miaka 17 tu, lakini Garrincha alidaiwa kuwa na kipaji kikubwa kuliko Pele. Ndani ya kipaji chake alikuwa pia mwehu mzuri tu. Kwa mfano, katika fainali za mwaka 1958 pale Stockholm baada ya Brazil kuichapa Sweden 4-2 na kutwaa Kombe la Dunia, Garrincha hakujishughulisha sana kushangilia. Wenzake walikuwa bize wakishangilia lakini yeye hakuelewa vizuri. Alijua mechi za Kombe la Dunia zingechezwa kama mechi za ligi kwao Brazil na timu yao ingepaswa kurudiana na timu zote ambazo walicheza nazo.

Umeshangaa kuhusu hilo? Basi haujashangaa sana. Garrincha alikuwa mtu wa ovyo. Mlevi, mhuni na asiyejijali sana. Alianza kuharibika akiwa na miaka 14 tu. Kwa mara ya kwanza kufanya mapenzi alifanya mapenzi na mbuzi. Ndiyo, mbuzi huyuhuyu mnyama unayemjua.

Garrincha alikuwa malaya mzuri na asiyejijali. Alimuoa mrembo mwanamitindo Elza Soarez ambaye alizaa naye watoto watano, lakini kwa jumla alikuwa na watoto 14 wa mama mbalimbali. Huyu ndiye Garrincha aliyekuwa na kipaji kikubwa.

Mwaka 1969 alimuua mama mkwe wake kwa bahati mbaya baada ya kuendesha gari akiwa amelewa na kuliingia lori lililokuwa limepaki huku mama mkwe wake akiwa mmoja kati ya abiria wake.

Garrincha alifariki dunia mwaka 1983 akiwa na miaka 49 tu. Alifariki kwa ulevi. Alifariki akiwa hana hata shilingi katika akaunti yake ya benki. Wabrazil waliendelea kumheshimu kwa kile alichokuwa akikionyesha uwanjani na kutwaa nao Kombe la Dunia mara mbili, lakini nje ya uwanja alikuwa kasheshe kubwa.

Nimemkumbuka Garrincha baada ya kumwona mchezaji anayeitwa Ronaldinho Gaucho akiwa ametiwa pingu Paraguay majuzi huku akienda mahakamani. Nikamkumbuka zaidi Garrincha baada ya kumwona tena Ronaldinho akiwa ndani ya gereza akiwa analewa huku akisaini katika fulana na vitabu vya kumbukumbu za mahabusu wenzake. Kwa nini Ronaldinho yupo ndani? Eti ameshikwa na pasipoti feki. Ametumia pasipoti feki ya Paraguay baada ya pasipoti yake ya Kibrazil na ile ya Kihispaniola kuchukuliwa na mamlaka za Wabrazil kutokana na kushindwa kulipa kiasi fulani cha pesa baada ya kuanzisha mradi wa kitapeli nchini kwao. Garrincha alitajwa kuwa mchezaji mwenye upeo mdogo wa kufikiria nje ya uwanja, pia jiulize kuhusu Ronaldinho. Mchezaji mwenye sura yake, anaweza vipi kusafiria pasipoti ya nchi nyingine bila ya watu kuhoji? Alitegemea nini?

Ni kweli Michael Jordan anaweza kusafiria pasipoti bandia ya Uingereza? Lionel Messi anaweza kusafiria pasipoti bandia ya Brazil? Venus William anaweza kusafiria Pasipoti feki ya Hispania.

Labda kuna watu wanaweza kufanya hivyo lakini sio watu wenye sura za kina Ronaldinho, Messi, Cristiano Ronaldo na wengineo.

Hata hivyo, kwa sasa Ronaldinho ana mikasa mingi ya ajabu nje ya uwanja. Kwa taarifa yako kuna mastaa wengi wenye vipaji vikubwa ambao wanatuangusha kama Ronaldinho. Mastaa ambao Mungu aliwapa vipaji vikubwa lakini nje ya mchezo uliowapa umaarufu wamejikuta wakiwa hawana maarifa ya kuwa watu wema.

Tangu wakati anacheza soka Ronaldinho alikuwa mtu wa ovyo. Mlevi na mpenda wanawake. Kwa sasa anakaribia kufilisika.